Search This Blog

Wednesday, December 21, 2022

HADITHI YA MVUVI MASKINI




    19-12-28T14:31:20.146+03:00








    Hapo zamani za kale aliishi mvuvi masikini ambaye kwa jina aliitwa Majuto. Majuto aliishi kwenye kijiji

    kidogo pembeni mwa ziwa dogo pamoja na familia yake. Kwa miaka mingi sana watu wa kijiji hicho

    walikuwa wakiishi wakitegemea ziwa hilo kwaajili ya samaki na maji kwa matumizi yao yote. Waliweza



    kukamata samaki wakuwatosha wao na pia wachache ambao waliweza kuuza kwenye vijiji vya jirani ili

    kujipatia mahitaji mengine.



    Kila asubuhi Majuto aliamka mapema na kutayarisha ngalawa na ndoano yake na kwenda kuvua samaki

    ili aweze kuipatia familia yake chakula. Ngalawa yake ilikuwa ni kubwa na imara sana yenye uwezo wa



    kwenda umbali mrefu juu ya maji bila tatizo lolote. Lakini Majuto alikuwa sio mvuvi mzuri kwa kuwa

    aliogopa sana maji na hakujua kuogelea. Kila siku aliwaza sana kabla ya kupanda ngalawa yake na



    alifikiria itakuwaje kama ikizama au ikipata shida ya aina yeyote na akadumbukia kwenye maji. Ni kwa

    sababu tu alikuwa hana njia nyingine ya kujipatia yeye na familia yake chakula ndio alilazimika kwenda



    na kuvua samaki. Rafiki zake Majuto walijaribu kumfundisha jinsi ya kuogelea lakini kila alivyoweka tu

    mguu wa kwanza ndani ya maji alihisi kama vile anazama na aliamua kukimbia. Kweli tatizo lake la

    kuogopa maji lilikuwa ni kubwa na ni sugu.

    Kila asubuhui Majuto alienda na ngalawa yake kuvua samaki lakini aliishia tu kutega ndoano yake



    kandokando mwa ziwa ambapo hapakuwepo na samaki wengi. Alifanikiwa kumkamata samaki mmoja

    mmoja tu na ndoano yake na mwisho wa siku alikuwa amekata jumla ya samaki watatu au wanne tu

    wadogo. Hili jambo liliendelea kila siku, aliondoka asubuhi na mapema na alirudi jioni na samaki



    wachache sana. Uwoga wake wa maji ulimsababisha asiweze kufanikiwa zaidi kama walivyo fanya

    wavuvi wengine ambao waliweza kwenda umbali mrefu zaidi na kukamata samaki wengi zaidi

    waliokuwa wakubwa.



    Masikini Majuto siku zilivyopita uwonga wake haukupungua na alibakia kuwaza sana jinsi atakavyofanya

    ili aweze kupata samaki wengi zaidi. “Jamani jamani, nitafanya nini masikini mimi. Mbona wenzangu

    wanafanikiwa na mimi nashindwa”, alilalamika Majuto. Aliwaza sana mpaka ghalfa wazo lilimjia –



    “nitaenda kumuomba mchawi anisaidie na kuniondolea shida zangu zote”, alisema Majuto. Pamoja na

    kuwa alishasikia kwa wazee wa kijijini na pia kwa watu wengi kuwa mchawi huyo aliyekuwa akiishi



    milimani sio mtu mzuri, Majuto hakufikiri mara mbili. “Hii ndio nafasi yangu kubwa ya kuweza

    kubadilisha maisha yangu kabisa. Hao wanaosema kuwa hili sio jambo zuri hawapendi kuniona

    nimefanikiwa”, alisema Majuto.





    Siku ikawadia na Majuto alifungasha virago vyake, aliiaga familia yake na kubeba zawadi ambazo alikuwa

    amemtayarishia mchawi. Bila kugeuka aliondoka upesi na kuelekea juu milimani alipokuwa akiishi huyo



    mchawi. Safari ilikuwa ni ndefu lakini Majuto alikuwa akitembea upesi sana. Alivuka mito, mabonde na

    misitu minene ambamo walikuwa wakiishi wanyama wengi wakali. Baada ya kutembea kwa muda mrefu

    Majuto alijikuta akipita kwenye uwanja mkubwa na kwa ghafla alitokea ndege mkubwa sana angani.



    Alikuwa na rangi ya zambarau na njano na mkia mrefu wa kuvutia. Majuto alishtuka sana alivyomuona

    huyo ndege kwa kuwa hakuwahi tena kuona ndege mkubwa hivyo aliyeruka angani. Alisimama mdomo

    wake ukiwa wazi kwa mshangao. Ndege huyo alitua chini ardhini na alizidi kumsogelea Majuto. Jasho



    jembamba lilimtoka Majuto na hakujua cha kufanya na alibaki amesimama tu bila kusema neno lolote.

    Ndege alisimama na kumuangalia Majuto machoni kisha akasema kwa sauti nzito, “Mtaka vyote hukosa

    vyote”. Kisha ndege aligeuka na kuruka angani na kupotea juu ya mawingu. Majuto hakuamini



    alichokiona na kusikia na alijihisi anaota. Alijaribu kutafakari lakini alikosa jibu na akaamua aendelee na

    safari yake ya kwenda kwa mchawi.



    Baada ya kutembea kwa muda mrefu Majuto hatimaye alifika kwenye nyumba aliyoishi mchawi. Ilikuwa

    ni nyumba kubwa nyeupe iliyovutia sana. Mawe meupe yaliyo ng’aa yalikuwa yamepangwa vizuri



    kuelekea hadi mlangoni. Majuto alikuwa anauoga lakini alijikaza na akagonga mlango. ”Nani wewe?”,

    alisikia sauti ikitoka ndani ya nyumba. ”Ni mimi Majuto mvuvi masikini. Nimekuja kuomba msaada



    wako”. Mlango ulifunguliwa na hapo alikuwa amesimama mzee mmoja mfupi mwenye mvi nyingi.

    Alionekana ni mtu wa kawaida tu tofauti kabisa na hadithi zote alizokuwa amezisikia Majuto huko kijijini

    kwake. Majuto aliwaza kuwa labda amekosea nyumba na huyu sio yule mchawi ambaye watu walikuwa



    wakimsema. Ikabidi Majuto amulize ”je, wewe ndio mchawi?”. ”Ha ha ha” alicheka mzee, ”ndivyo watu

    wanapenda kuniita hivyo. Karibu sana ndani”.



    Majtuo aliingia na kukaa chini kwenye mkeka. ”Ninaweza kukusaidiaje?” aliuliza mchawi. ”Nimefunga

    safari kutoka mbali kuja huku ili niombe msaada wako”, alisema Majuto. ”Mimi ni mvuvi lakini



    ninaogopa sana maji na hivyo inanizuiya kuweza kwenda mbali na ngalawa yangu ili nikatege ndoano

    yangu na kukamata samaki. Kila ninavyowaza jinsi ya kufanya nashindwa na ninabakia tu kando kando



    mwa ziwa ambapo samaki ni wachache na pia ni wadogo. Ninakuomba sana unisaidie kuondoa uwoga

    wangu wa maji ili niweze kujifunza kuogelea na kupata uhodari wa kwenda mbali zaidi na ngalawa



    yangu.” ”Lo, nimekuelewa”, alisema mchawi. ”Tatizo lako ni dogo sana. Subiri hapa nitakuletea dawa

    itakayo kusaidia”. Mchawi aliamka na kwenda uwani. Baada ya muda si mrefu alirudi huku ameshika

    chungu kidogo chenye kilichofanana na maziwa. Alimpa Majuto kile chungu na kumwambia anywe.



    Majuto alifanya hivyo. Baada tu ya kumaliza alisikia tumbo lake lina nguruma na mwili wote ulisisimka.

    Alianza kujisikia wa tofauti kama vile amekuwa mwepesi zaidi. Mchawi akamwambia Majuto, " Hii dawa

    imekufanya uwe mwepesi na kuanzia leo utaweza kuogelea bila ya kuzama". Majuto alifurahi sana na



    kumshukuru mchawi kwa msaada wake. Kuonyesha shukurani yake Majuto aliitoa zawadi yake

    aliyomletea na kumpa.



    Wakati wa kuagana ulipofika Majuto alikuwa tayari kuondoka. "Asante sana mzee, sasa mimi nitarudi

    kjijini kuendelea na maisha yangu", alisema Majuto. "Ngoja kidogo." Alisema mchawi. "Kwani wewe

    usingependa nikuwezeshe pia kukamata samaki wengi zaidi? Kwanini nisikupe kifaa ambacho



    kitakuwezesha kukamata samaki wengi sana?" Majuto hakuamini alichosikia. "Mzee, yaani kuna kifaa

    ambacho kitaniwezesha kukamata samaki wengi zaidi?", alisema Majuto. "Ndio, nitakupa lakini itabidi

    ukubaliane na masharti yangu kwanza", alisema mchawi. "Niambie tu na mimi nitayatekeleza", alisema

    Majuto.



    Mchawi aliondoka tena kuelekea uwani na kurudi na nyavu kubwa. Majuto hakuelewa ni nini kile

    alichokuwa amekishika mchawi kwa kuwa hakuwahi kuona nyavu maishani mwake. Siku zote yeye na

    wavuvi wenzake walikuwa wakitumia ndoano tu kuvulia samaki na hawakujua nyavu ni nini. Mchawi



    akasema, "Hii ni nyavu. Iweke ndani ya maji kila jioni, utakapo rudi jioni utakuta samaki wengi sana

    wamenasa kwenye matundu. Kazi yako itakuwa ni kuwaokota tu na kuwaweka ndani ya ngalawa yako."

    Majuto hakuamini masikio yake. "Kweli hii ni siku ya furaha sana maishani mwangu. Lakini kwanini

    unataka kunifanyia haya yote?" aliuliza Majuto. Mchawi alimjibu, "Hapo zamani niliwakosea watu wengi



    na nilifanya mambo mengi mabaya. Ndio maana ilinibidi nikimbilie na kuishi mwenyewe huku milimani.

    Lakini nimefikiria sana mambo niliyoyafanya na nimeyajutia ndio maana ninataka kuwasaidia watu.

    Sitakuomba mengi, lakini kila utakapoenda ziwani kuvua samaki ninataka uchukue nusu ya samaki wote



    uliowashika na kuwapa masikini na wazee wasiojiweza. Ukishindwa kuyatekeleza haya basi na wewe pia

    hautafanikiwa" Majuto haikumbidi hata kufikiria sana na alijibu, "Mimi pia ninapenda sana kwasaidia

    watu lakini tu sikuwa na uwezo. Sasa umeniwezesha na mimi pia nitawasaidia watu wengine zaidi ya

    hata uliyoniambia."



    Kwa maneno hayo waliagana, na Majuto alibeba nyavu aliyopewa na mchawi na kuelekea tena kurudi

    nyumbani. Alikuwa na furaha kubwa sana na alikimbia upesi sana hadi kufika nyumbani kwake.

    Hakuwaza hata kusimama na kusalimia familia yake na kuwaambia kuwa amerudi, alikimbia moja kwa



    moja hadi kwenye ziwa na kujitupa kwenye maji. Na kweli mchawi alivyokuwa amesema Majuto

    hakuzama. Alibaki tu juu ya maji akielea. Majuto alishangilia sana na kwenda kuwatangazia rafikiki zake



    wote yaliyomkuta. Nao pia wakabaki kufurahi naye kwasababu Majuto alikuwa ni rafiki yao wa siku

    nyingi.



    Jioni ilivyofika na wavuvi wengine wakiwa wanarudi majumbani mwao, Majuto ndio alianza kuandaa

    ngalawa yake. Alizipandisha nyavu alizopewa na mchawi huku akitabasamu. ”Leo ndio maisha yangu

    yanabadilika, shida zangu zote ninaziacha nyumba”, alisema Majuto. Alipanda ndani ya ngalawa yake na



    kuondoka kuelekea ziwani. Giza lilikuwa linaingia taratibu lakini Majuto hakuwa na wasiwasi kabisa na

    alizidi kwenda mbali. Baada ya kusogea kwa muda, miti iliyokuwa ikiota kando mwa ziwa ilizidi



    kuonekana midogo. Nyumba za kijiji nazo zilizidi kuonekana ndogo alivyozidi kwenda mbali. Alikuwa

    amebakia mwenyewe tu kwenye ziwa, watu wote walikuwa wamesharudi majumbani kwao na

    kupumzika kwa siku hiyo.



    Ghafla Majuto alisikia mlio wa ndege ikitoka angani. Aligeuka kwa haraka na kuangalia juu. Ilikuwa ni

    kama ndoto imejirudia, yule ndege mkubwa aliyejitokeza kwenye safari yake ya kwenda kwa mchawi

    alikuwa amerudi. Majuto aliogopa sana kwa kuwa alijua yuko peke yake na hakuna mtu wa kumpa



    msaada wowote. Ndege alizunguka ngalawa mara mbili halafu akatua juu ya yake. Walibaki

    wanaangaliana tu kwa muda mrefu kisha ndege akafungua mdomo akasema, ”Mtaka vyote hukosa

    vyote”. Kisha ndege aligeuka na kuruka angani na kupotea juu ya mawingu. Majuto alibaki tena kuwaza



    sana nini maana ya hayo maneno. Kwanini ndege amwambie kuwa akitaka vyote atakosa vyote? ”Mimi

    sina tamaa”. Alisema Majuto. ”Kwa hivyo ninajua kuwa sitaweza kupata shida ambazo ameniambia

    ndege”.



    Basi Majuto aliendelea hadi sehemu ambapo wavuvi wengine walisema kuwa kuna samaki wengi.

    Alishusha nyavu ndani ya maji kama mchawi alivyokuwa amemwelekeza. Nyavu zilikuwa ni nyepesi na

    alifanikiwa kuziweka ndani ya maji bila ya kupoteza muda. Alibaki kusubiri hapo hapo mpaka giza

    likaingia bila ya kitu chochote kutokea. ”Mchawi aliniambia kuwa nitakamata samaki wengi sana lakini



    Mbona hakuna dalili yeyote hapa?”, alisema Majuto. Masaa yalizidi kusogea na giza lilitanda lakini

    Majuto alivumilia huku akisubiri ishara yoyote kuwa kuna samaki amekamatwa lakini hapakutokea kitu.

    Usingizi ulianza kumshika Majuto na baada ya muda si mrefu alisinzia.



    Mjuto hakuamka mpaka pale ambapo jua linaanza kuchomoza upande wa pili mwa ziwa. ”Kweli

    nimehangaika bure”, alisema Majuto. ”Nimekesha usiku mzima na hakuna samaki hata mmoja.” Kwa

    huzuni kubwa alianza kuzivuta nyavu iliazirudishe kwenye ngalawa. ”Mbona nyavu zimekuwa nzito

    sana?”, alijiuliza. ”Au ni kwa kuwa zimeloa?”. Alizidi kuvuta kwa nguvu zake zote ndio nyavu zikaanza



    kupanda taratibu. Majuto aliangalia kwa makini zaidi na alishtuka kuona kuna samaki mmoja amekwama

    kwenye nyavu. Alizidi kuvuta nyavu na mara akaonekana samaki mwengine mkubwa zaidi naye

    amekwama kwenye nyavu. Majuto alizidi kufurahi na kuvuta nyavu kwa nguvu zaidi. Kila akizivuta na



    samaki wengi wakubwa walikuwa wakizidi kupanda juu. Majuto alishangilia kwa sauti kubwa na kupiga

    kelele kwa furaha. Alimalizia kupandisha nyavu na kuanza kuhesabu samaki. Walikuwa ni wakubwa na

    wengi sana mpaka alishindwa kuhesabu wote. Majuto hakupoteza muda, aligeuza ngalawa yake na

    kuelekea kurudi kijijini.



    Majuto alipokaribia kufika aliiona familia yake na rafiki zake wengi wakimsubiri kando ya ziwa.

    Aliwapungia mkono kuwaonyesha kuwa kila kitu kilikuwa ni salama. Kweli ilikuwa ni siku ya furaha

    kubwa kwa Majuto na familia yake yote. Majuto aliwapa rafiki zake wote samaki. Pia aliwapa masikini na



    wazee wasiojiweza kama mchawi alivyokuwa amemwelekeza Majuto. Watu wote siku hiyo walifurahi

    kwa pamoja. Pamoja na kwamba alikuwa amewapatia ndugu na marafiki samaki wengi bado alikuwa

    amebakiwa na wengine wengi. Majuto alipeleka samaki waliobaki sokoni na kuwauza kwa bei nzuri sana

    na kupata fedha nyingi.

    Maisha ya Majuto na familia yake yalibadilika. Kila jioni Majuto alienda ziwani na kutega nyavu zake na



    kurudi asubuhi na samaki wengi sana. Nusu ya samaki wote aliokamata aliwapa masikini na wazee,

    baada ya hapo alienda sokoni na kuuza samaki waliobaki kwa faida kubwa. Haikuchukua muda mrefu na

    Majuto alipata uwezo wa kujenga nyumba kubwa ya kifahari yenye vyumba vingi. Nje alipanda bustani



    kubwa ya maua na kufuga wanyama na ndege wengi wa kifahari kutoka nchi za mbali. Pia alikuwa na

    wafanyakazi wengi wa ndani ambao walifanya kazi zote za ndani ili mke wake na watoto wake wasipate

    taabu yeyote. Majuto alianza kujivuna na mali zake na hatimaye aliamua kuwa kazi ya kwenda ziwani



    kila siku kukamata samaki haimfai yeye, aliamua kuajiri vijana wachache wakufanya hiyo kazi. Kweli

    maisha yake na familia yake yalikuwa ni mazuri.



    Usiku mmoja Majuto alikuwa amelala kitandani ndoto ikamjia. Aliota kuwa yuko kwenye chumba kidogo

    kisichokuwa na madirisha wala milango. Alijaribu sana kutoka lakini alishindwa. Ghalfla yule ndege

    mkubwa ambaye Majuto alishakutana naye mara mbili alitokea. Ndege alibaki tu anamwangalia Majuto



    kisha akasema, "Mtaka vyote hukosa vyote." Kisha ndege akapotea. Majuto aliamka kwa mshituko

    mkubwa lakini alivyojua kuwa ni ndoto tu alitulia kidogo. "Lah, kumbe ni ndoto tu." Alisema Majuto.



    Alitafakari ndoto yake kwa muda mfupi lakini hakuona kama vile ni jambo lolote la kushitua na akarudi

    kulala. Kesho yake maisha yaliendelea kama kawaida.





    Lakini haikuwa ni rahisi kutunza vyote hivi mwenyewe na kisha ilimbidi Majuto kuajiri wafanyakazi wengi

    wa kutunza nyumba na mali zake zote. Pia Majuto alianza kuwa na wasiwasi juu ya usalama wake.



    Alifikiria kuwa kama haya yote yametokana na yeye kuwa na nyavu, je nyavu hii ikipotea au ikiibiwa,

    itakuwaje? Basi aliamua kuajiri walinzi wengi pia wakumlinda yeye na mali zake zote. Walinzi wengine

    aliwaajiri kwa kulinda nyavu tu.



    Pamoja na mali zake zote Majuto alizojikusanyia, bado alikuwa anataka mengine mengi. Alitaka awe na

    nyumba kubwa zaidi na ya kifahari zaidi. Alipenda awe na wanyama wengi wa kutoka nchi za mbali zaidi

    na wafanyakazi wengi zaidi. Pia alitaka aweze kusafiri nchi za mbali na aweze kurudi na zawadi nyingi

    kwa ajili ya familia yake.



    Mali za majuto zilivyozidi kuwa nyingi na taabu na mawazo yalizidi kuwa mengi. Gharama za kulipa

    wanfayakazi wake wote zilizidi na baadala ya kufurahia maisha yake mazuri alianza kuwaza sana. “Haya

    yote nitaweza kuyatekeleza kweli iwapo nusu ya kipato changu chote nitaendelea kuwapa masikini?”



    Alisema Majuto. “Hata hivyo nimeshawasaidia vya kutosha. Kuanzia sasa itabidi nianze kujifikiria

    mwenyewe na matakwa yangu.” Kuanzia siku hiyo Majuto aliamua kuwapa masikini robo tu ya mapato

    yake. Majuto alifikiria, “Mchawi kweli aliniambia niwape masikini nusu ya mapato yangu yote, lakini kwa



    sasa ninadhani nimeshawasadia vya kutosha. Kwani mchawi atajuaje kuwa siwapi masikini nusu ya

    mapato yangu.” Kufanya hivi kulimwezesha kuendeleza maisha yake ya kifahari. Alijenga nyumba kubwa

    zaidi na kuajiri wafanyakazi wengi zaidi. Pia alisafiri mbali zaidi na kurudi na zawadi nyingi zaidi kwa

    familia yake.



    Lakini kama ilivyokuwa mara ya kwanza, gharama za kutunza mali zake zote zilizidi kuwa kubwa.

    Hatimaye Majuto aliamua kuwapa masikini robo ya mapato yake haitawezekana tena. Aliamua kuwa

    kuanzia sasa yeye mwenyewe ndio atakayefaidika na kazi yake. Aliacha kabisa kuwasaidia masikini na



    wazee na pia tabia yake ilibadilika. Majuto hakuwa tena mtu mwenye roho nzuri kama watu

    walivyokuwa wakimfahamu. Alibadilika na kuwa mtu mwenye hasira za haraka na alibaki kugombana



    sana na watu, hata rafiki zake wa karibu. Mtu yeyote mwenye shida akimfuata Majuto alikataa kabisa

    kumpa msaada hata kama alikuwa na uwezo wa kufanya hivyo. Mara nyingine alitumia hata walinzi

    wake kuwafukuza watu hao wenye shida.





    Siku moja Majuto alikuwa akitembea kwenye bustani yake alitokea bibi kizee mmoja na kumwambia

    Majuto, “Tafadhali sana naomba unisaidie nimepata shida. Nyumba yangu ambapo nilikuwa nikiishi na

    mtoto wangu mmoja na mjukuu wangu imeshika moto na kuteketea kabisa. Sina pakuishi wala chakula.



    Ninakuomba unisaidie kwa lile utakalo weza.” Majuto alicheka kwa sauti kubwa, “ Ha ha ha, wewe bibi

    kizee unatembelea magongo hata nikikusaidia wewe utaweza kunisaidia nini.” Hapo sauti ya Majuto

    ilibadilika na aliongea kwa ukali sana, “Ondoka upesi sana hapa na usirudi tena! Nyie watu mnakuwa



    hamna shukurani kabisa. Muda wote huu nimewasidia lakini mpaka leo mnaendelea tu kuja kwangu

    kuomba misaada. Ondoka haraka na usirudi tena.” Masikini bibi kizee alianza kuondoka kwa

    kunyong’onyea.



    Ambacho Majuto alikuwa hajaona ni kuwa juu ya mti mkubwa uliokuwa kando yake yule ndege mkubwa

    alikuwa amekaa na anaona yote yaliyokuwa yakitokea. Alitoa kelele kubwa kwa hasira “Ng’waaaa!”

    Kisha ndege huyo aliruka na kutua mbele ya Majuto na kuongea. “Majuto, nimekupa kila ulichotaka na



    kukuongezea mengine mengi. Sharti lilikuwa ni moja tu. Wape masikini na wasiojiweza nusu ya mapato

    yako. Lakini hili umekuwa na tamaa na kusahau watu wengine.” Kwa maneno hayo ndege aligeuka na

    alibakia hapo amesimama mchawi. Kumbe siku zote hizo Majuto hakujua kuwa yule ndege ndio mchawi.



    Alikuwa amejigeuza ili aweze kumkumbusha majukumu yake kama tajiri. Lakini Majuto alizidiwa na

    tamaa na kuamua kutojali watu wenye shida. “Mtaka vyote hupoteza vyote. Na wewe leo umepoteza

    vyote. Hili liwe onyo kwako. ” Alisema mchawi.

    Upepo mkali ulianza kuvuma kwa ngurumo mkubwa na vumbi lilitimka. Ardhi yote ilitetemeka na miti



    ilitikisika. Majuto alifunga macho na kuziba masikio kwa uwoga. Baada ya muda mfupi upepo uliisha na

    kila kitu kilitulia. Majuto alifungua macho yake taratibu na kuangalia huku na kule. Alidhani kuwa

    amehamishwa kwenda sehemu nyingine. Nyumba yake na bustani na mali zake zote zilikuwa



    zimetoweka. Mchawi naye pia alikuwa ametoweka. Kilikuwa kimebakia tu kibanda alichokuwa akiishi

    zamani. Alianguka chini na kutoa kilio kikubwa.

    Majuto aliamka tena na kutembea taratibu kwa kujivuta mpaka kwenye banda lake na kuchungulia



    ndani. Aliona familia yake bado ilikuwepo na wote walikuwa wazima. Aliweza kusikia amani kidogo kuwa

    hao bado walikuwa ni wazima. Majuto aliingia ndani ya banda na kutazama vizuri huku machozi bado

    yanamtoka. Alishtushwa kuona kuwa bado nyavu alizokuwa amepewa na mchawi zilikuwa zimelala

    kwenye mkeka.





    “Hili litakuwa ni fundisho kwangu.” Alisema Majuto. Pamoja na masikitiko yake yote Majuto alikuwa

    amejifunza kitu cha muhimu sana. Tamaa ya mali inakufanya usifikirie kuhusu shida za watu wengine.



    Inabidi kumsaidia mtu mwenye shida pale unapoweza bila kubagua. Kuanzia siku hiyo Majuto alianza

    kujenga maisha yake upya lakini alibaki kukumbuka maneno aliyokuwa akimkumbusha kila mara,



    “Mtaka vyote, hupoteza vyote.” Na mpaka leo hii Majuto anaishi maisha mazuri sana kando mwa ziwa

    na familia yake wakipendana na kusaidiana na watu wote wengine.



     (MWISHO WA HADITHI).

0 comments:

Post a Comment

BLOG