Alikuwepo mtu mmoja ambaye
alikuwa mvivu kupita kiasi, alikuwa akipenda kulala tu na pengine hupita
mikahawani na kupiga masoga. Mtu huyo, vile vile, alikuwa na tabia ya uchafu wa
kiwiliwili chake na nguo pia. Hakupenda kufua nguo, kukoga, kukata makucha wala
kusafisha meno yake. Alikuwa mtu yeyote hapendi kumtupia macho kwa hali ya
uchafu wake. Watu wa hapo kwao wakifanya kazi za kulima chakula chao na pesa za
matumizi ya mambo mengine pia zilikuwa zikitoka humo humo katika vipando vyao.
Mtu huyo mvivu alikuwa na tabia ya kupita katika vijumba vya wenziwe na kudusa.
Alikuwa akijuwa wakati wa kila mtu anapokunywa chai au anapokula chakula cha
mchana au kijio. Akijua kuwa, sasa mtu fulani yu tayari kula, huko kwake, basi
atakwenda ajidai kutoa masoga mpaka akaribishwe kula. Hii ndiyo iliyokuwa tabia
yake na hivi ndivyo alivyokuwa akiishi. Watu wa hapo kwao walianza kukirihika
kwa tabia yake hii mbaya na kila mtu alikuwa akimsema na kumdharau. Yeye
mwenyewe alitambua kuwa watu wanaudhika naye, sababu baadhi ya watu, wale
machope machope, walikuwa wakimwambia, 'Eh, baba wee, kazi yako ni kupita
majumbani na kudusa tu, hufanyi kazi!!' Yule mtu hakuwacha tabia yake kwani
alipokuwa akienda kule majumbani kwa watu mahashumu yaani watu wenye haya na
tabia nzuri, walikuwa wakisema naye vizuri, na kuchekacheka naye, basi aliona
haudhi mtu. Lakini juu ya hivyo hata wale watu mahashumu hawakupenda tabia yake.
Kwa muda kupita ulianza mnong'ono mjini, watu wote pamoja walifanya shauri kuwa
mtu huyo akomeshwe tabia hii ya uvivu, ya kupita majumbani mwa watu na kudusa.
Katika mkutano huo wa watu palikubaliwa na watu wote kuwa wamwendee watu wawili
wamwambie kuwa watu wote hawaipendi tabia yake mbaya hii, na ya kuwa ni lazima
afanye kazi kama watu wengine na asipofanya hivyo watu wote wa hapo kwao
hawatamsaidia kwa chakula. Walimwendea watu wawili wasiokuwa na muhali yaani
wasiokuwa na haya. Walimkuta mkahawani anapiga soga na huku ana kipande cha
andazi mkononi anakinyofoa nyofoa. Kiandazi hicho alikiomba kwa mtu aliyekuja
hapo mkahawani na kununua kikombe cha tangawizi na andazi moja. Wale watu wawili
walimwita siri na walianza kumwambia kuwa watu wa hapo kwao wamewatuma wamwambie
aache tabia ya uvivu aende akalime kama watu wengine na aache kupita vijumbani
akidusa na ya kuwa tokea siku ile hatapewa chakula na mtu yeyote. Alipoambiwa
maneno haya yule mvivu, alipuuza, akajichekesha na kurudi hapo mkahawani na
kuendelea na sogalake. Wakati wa chakula cha mchana ulipofika, alianza kazi yake
ya kuranda. Alikwenda kwa mtu wa kwanza akakuta watu wanapakuwa. Hapo alikaa na
kujikuna kuna kichwa na huko yumo katika kutoa porojo lake la desturi. Mwenye
nyumba alimwambia, 'Jana tulikutumia fulani na fulani, hawakukwambia maneno ya
watu wa mji?' Hapo alinyamaza kimya, hakujibu. Hapo yule mwenye nyumba alifunga
mlango wake na huku anamwambia, 'Haya baba, kwa heri.' Lile vivu lilikwenda zake
na akaona, hakika mambo yamemharibikia. Alijaribu tena kwenda nyumba nyingine,
alipofika huko watu wanakosha mikono ili wapate kula, naye alinyoosha mkono wake
atiliwe maji ya kunawa, lakini mtia maji hakumtilia na aliona haya sana. Hapo
hakuambiwa neno wala hakukaribishwa bali watu waliinama na kuendelea kula tu.
Hapo vivu lilinyerereka likaenda zake na huku analia kwa njaa. Watu wa nchi hiyo
walikuwa wakarimu sana lakini walifanya hivyo kwa kutaka kumuelimisha mwendo
mzuri wa kibinadamu. Njaa ilipomshika barabara, lile vivu ilimjia fikira aende
kwa mtu yeyote akamuombe kazi apate chakula badala ya kuomba chakula. Basi
alikwenda kwa Mwarabu mmoja wa Maskati aliyekuwa akiweka duka hapo kwao na
kumwambia ampe kazi. Yule Mwarabu alikuwa hajui kusema Kiswahili vizuri, basi
alimjibu, 'Kama nataka kazi, tasafisha haba mbele ya nyumba wangu, khalafu
tashkuwa ndoo na kwenda kwa mtoni nashkuwa maji naleta, taumba senti khamsini.'
Yule mvivu alijikaza na akaifanya ile kazi ya kusafisha mbele ya nyumba ya yule
Mwarabu na kwenda mtoni kuchukua maji akapewa, senti khamsini. Hapo alijinunulia
nusu kibaba cha mchele na nguru wa senti kumi akaenda akajipikia akala akashiba.
Alipokwisha kula, ilimjia ari na fikira ya maisha yake mabaya, alisema moyoni
mwake kuwa ni lazima ajisaidie kwa kufanya kazi, hataki tena kudusa wala
kutamania mtu yeyote. Hapo alifanya kazi ndogo ndogo hapo mjini kwao na huku
anadunduliza vipesa hata akapata shilingi nne akazinunulia jembe la kulimia.
Basi aliacha tabia ya uvivu na alianza kufanya kazi. Alikwenda kwenye kisitu
alichokirithi kwa mama yake, akaanza kukifyeka na kupanda kila namna ya vitu.
Alipanda mtama, mahindi, mboga, matango na vyenginevyo. Mungu alimbarikia
akavuna vitu vingi sana akavijaza ndani ya kibanda chake na ikawa hahitaji kitu
cho chote cha mtu. Siku zote alikuwa yakimjia majuto ya maisha yake ya nyuma na
akijilaumu sana kuishi maisha yale ya kivivu na fedheha. Mavuno yake yalipokuwa
makubwa, yaani yalipomzidi hata ikawa hawezi kuyala peke yake, alichukuwa baadhi
ya vitu kama vile mahindi na mboga na kuvipeleka sokoni kuviuza. Watu
walipomuona huko sokoni, hawakupenda kununua vitu vyake kabisa kwa sababu ile
tabia yake ya uchafu hakuiacha bali alizidi kuwa mchafu tokea alipoanza
kujishughulisha kwa kazi za kulima. Huko sokoni alipambana na mtu mmoja
aliyependa sana mboga zake lakini alipomuona mwenye mboga alisema, 'Oh, sipendi
mboga zako, sababu wewe u mchafu. Nenda kakoge, ufue nguo zako na ukate makucha
yako, halafu unaweza kuja kuuza vitu vyako na watu wanaweza kuvinunua.' Yule mtu
alijilaumu sana kwa kujiweka mchafu. Kwa hivyo alianza kujinadhifisha na
kujiweka katika hali nzuri. Mara ya pili alipeleka tena vitu vyake sokoni, watu
walipomuona huko walimfurahikia sana kwa unadhifu wake na vitu vyake vizuri.
Aliuza vitu vyake kwa bei nzuri sana na alirudi kwake na pesa chungu nzima. Huyo
mtu alitanukiwa na maisha yake haya mapya. Aliendelea kufanya kazi na kuuza vitu
sokoni hata akawa na pesa nyingi sana. Hapo alijenga nyumba nzuri na kununua
nguo nzuri. Basi aliishi maisha ya raha na furaha kama wenziwe au zaidi. Mtu
huyo asingelipata raha hiyo lakini alipopigwa na njaa alifundishika, akaanza
kufanya kazi na vitu vyake vilipokataliwa huko sokoni, vile vile, alifundishika
akaacha tabia ya uchafu. Kwa hivyo ni kweli wanayosema watu kuwa ukupigao ndio
ukufunzao.
Menu
Blog Archive
-
▼
2022
(50)
-
▼
December 2022
(50)
- HADITHI YA MVUVI MASKINI
- Ukupigao Ndio Ukufunzao
- Mshika Mawili Moja Humponyoka
- Mchimba Kisima Huingia Mwenyewe
- Simba Mwenda Pole
- Abunuwasi Na Mkono Wa Ajabu
- Wajinga Ndio Waliwao
- Abunuwasi Na Viatu
- Abunuwasi Na Hukumu Ya Kijana
- Abunuwasi Na Mlinzi
- Maji Yakimwagika Hayazoleki
- Mtaka Cha Uvunguni
- Ajali Haikimbiliki
- BINTI NURU
- IMANI YENYE KUFUFUA
- BINTI YANGU JOANITHA
- UA JEKUNDU
- SIKU MBAYA KAMA HII
- SARAFINA
- THE WICKED DEMAND (HITAJI LENYE UOVU)
- FAITHFULNESS
- HYUNG NIM
- JERAHA LA MOYO
- AMKA MAMA
- BINADAMU HATUNA UTU
- FADHILA
- NILIKATAA UCHUNGAJI NIKAWA MKUU WA WACHAWI
- NISINDIKIZENI KWA AMANI
- NATAMANI MAMA ANGERUDI HATA KWA DAKIKA TANO
- KWANINI MAMA…LAKINI KWANINI MAMA?
- BINAADAMU HATUNA FADHIRA
- KIFO CHA YATIMA DANNY
- KIJANA MCHOKOZI NA KICHAA
- KISA CHA BIBI MCHAWI
- MKONO WA FARAJA
- FUKARA WA FIKRA
- WATOTO 100
- NATAMANI MAMA ANGEKUA HAI NIMUOMBE RADHI
- JIJINI DAR ES SALAAM…!
- MSAMBWANDA !!
- KIPANDAUSO
- OMBA OMBA
- KAMANDA
- BALAA
- NILIFANYA BIASHARA YA VIPODOZI NA MISUKULE
- BARUA YA MTOTO KWA MAMA YAKE
- CHOZI LA MILELE.
- UWE SAUTI YAO
- JINSI YA KUIPATA FURAHA
-
▼
December 2022
(50)
-
►
2023
(147)
- ► January 2023 (147)
0 comments:
Post a Comment