Search This Blog

Monday, January 2, 2023

DADA YANGU

 






Mapenzi ni kitu ambacho kimechukua nafasi kubwa sana katika maisha ya watu kote duniani. Mapenzi haya yanaweza kuleta furaha sana endapo mtu atampata mtu sahihi ambaye atakuwa ni muwazi, mwenye mapenzi ya kweli na kuheshimu uhusiano huo. Lakini mapenzi yanaweza kuleta karaha au kukosa amani kabisa kama kutakuwa na migogoro ambayo unakuta inasababishwa na kukosa uaminifu na kuleta ugomvi kati ya wawili wapendanao. Mapenzi haya yanaweza yakasababisha ndugu kugombana, marafiki kukosana na hata kuuana.



*****

Eliza na Upendo ni wasichana warembo waliozaliwa katika familia ya kitajiri mkoani Morogoro. Wasichana hawa waliishi katika maisha ya kifahari kutokana na Baba yao Mzee Bondi kuwa na uwezo mkubwa sana kifedha. Mzee Bondi aliwapenda sana mabinti zake na alipenda wasome kwa bidii ili baadaye waje kuwa na maisha bora. Eliza na Upendo walisoma katika hali nzuri sana hadi kufikia elimu ya chuo, ambapo Upendo alikuwa akisoma Chuo Kikuuu cha Dar es Salaam na Eliza Chuo cha Uhasibu

Arusha. Kutokana na masomo walitengana na kuonana mara chache

kipindi cha likizo.

Baadaye Eliza na Upendo walijikuta wakijiingiza katika uhusiano wa

kimapenzi wote wawili kwa kijana mmoja mtanashati aliyeitwa James bila

kujijua. Uhusiano wa kimapenzi kwa mwanamume mmoja ulileta

migogoro katika familia yao.



*********

Baada ya kumaliza Kidato cha Sita Upendo alipangiwa kwenda kuendelea na masomo ya Chuo Mkoa wa Dar es Salaam. Baba yake alifurahi sana na kumuahidi kuwa angempa zawadi nono kama angefanya vizuri akiwa Chuo. Kabla ya kujiunga na chuo Upendo alifanyiwa sherehe kubwa ya kumpongeza, ambayo ilihudhuriwa na watu wengi sana ndugu jamaa na marafiki. Wakati huo mdogo wake Eliza alikuwa Kidato cha Sita kwani walipishana mwaka mmoja tu na kwa jinsi walivyokuwa, walionekana

kama mapacha. Wakati mwingine ilikuwa ni vigumu kwa watu ambao

walikuwa hawajawaona kujua mkubwa ni yupi na mdogo ni yupi. Siku zilipokaribia za kwenda Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Upendo alijiandaa barabara kwa ajili ya kuanza masomo ya Chuo. Siku moja kabla ya kuondoka Mama na Baba yake walimwita na kuzungumza nayemazungumzo ili kumwasa na kumpa ushauri.

“Upendo tumeishi wote kutoka ukiwa mdogo, hujawahi kuishi mbali nasi kuanzia masomo ya elimu ya shule ya msingi hadi elimu ya Sekondari. Umesomea Morogoro, sasa unakwenda Dar es Salaam kuanza maisha mapya ya kuishi mbali na sisi. Ninakuomba ukasome kwa bidii ili ujiandalie maisha yako ya baadaye.” Mzee Bondi alimaliza kutoa nasaha zake, huku Upendo akisikiliza kwa makini kabisa.

“Umsikilize baba yako kwa makini kwa sababu dunia ya sasa imeharibika mwanangu. Magonjwa ni mengi na ukifika huko sio ndio ukasahau kilichokupeleka. Kumbuka kinachokupeleka ni masomo na sio starehe. Nadhani umenielewa.” Alisisitiza Mama yake.

“Jamani Mama nitasoma kwa bidii mbona unaongea hivyo.” Upendo alihamaki “Lazima niongee mwanangu vijana wa sasa mnakutana na mambo mengi na vishawishi vingi usipokuwa makini utapoteza kabisa mwelekeo na malengo yako.” Mama upendo aliendelea kutoa nasaha.

“Baba na Mama nimewasikia, kamwe sitoenda kutenda yasiyo sahihi,

nitasoma na nitawafurahisha siku zote wazazi wangu.” Upendo alijibu kwa

unyenyekevu.

Baada ya maongezi hayo wote walisimama na kuelekea kulala ili Upendo akaanze kujiandaa na safari. Upendo aliingia chumbani na kuanza kupanga vitu vyake akisaidiana na mdogo wake Eliza.

“Ndugu yangu si nilikuwa nimekaa na Mama na Baba sebuleni wananipa wosia namna ya kuishi huko Chuo.” Alisema Upendo.

“Eheh! Ilikuaje? Kwa sababu Mama naye akiamua kuongea ni balaa wamesemaje hao wazee?” Alidadisi Eliza.

“Mwenzangu, Baba na Mama wameniambia nikienda nisisahau kilichonipeleka nisiendekeze starehe.” Alisema Upendo.

“Heh! Hao wazee nao inamaana ukakae tu unasoma hata disko usijichanganye? Aka mwaya sisi bado vijana lazima tujirushe we ngoja mi nimalize Kidato cha Sita nikienda chuo nitajirusha sana kwani hapa nyumbani hawa wazee wanatubania sana.” Alizungumza Eliza.

“Usiseme hivyo mdogo wangu mimi naona Baba na Mama wapo sahihi, kwani nikianza kujiingiza kwenye starehe nitajikuta nafeli mitihani halafu malengo yangu ya kuwa mwanasheria yasitimie, we mwenzangu unawaza kujirusha tu.” Alijibu Upendo.

“Kujirusha ni wajibu na kusoma nitasoma tu, haya bwana tufanye haraka tuwahi kulala hao wazee watakuamsha mapema kesho.” Alimaliza Eliza.

Kesho yake asubuhi na mapema Mama yake Upendo alimwamsha na kumshauri Upendo ajiandae kwani safari ingeanza saa nne asubuhi. Eliza siku hiyo hakwenda shule ili amsindikize dada yake. Walikunywa chai kwapamoja na tayari baba yao alikuwa amejiandaa kwa safari. Waliondoka na usafiri wao binafsi hadi Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na kumwacha Upendo. Upendo alimwaga mama yake na mdogo wake akiwa na huzuni kutokana na kuanza maisha mapya. Upendo alipangiwa kuishi katika hosteli za mabibo ambazo zipo kandokando ya barabara ya Mandela

upande wa kulia kutokea Ubungo kuelekea Buguruni.

Akiwa chuoni Upendo alikukutana na watu mbalimbali. Alijitahidi sana kusoma kwa bidii akiwa na uwezo mzuri darasani aliweza kufaulu vizuri mitihani yake.

Eliza naye alimaliza Kidato cha Sita na kupangiwa kwenda kusoma Chuo cha Njiro Mkoa wa Arusha wakati huo Upendo alikuwa amebakiza mwaka mmoja ili amalize Chuo. Upendo aliishi vizuri na alipendwa sana na wanafunzi kutokana na juhudi zake katika masomo na tabia yake nzuri aliyokuwa nayo, hivyo alikuwa na marafiki wengi na pia walimu walimpenda sana.

Wakati akikaribia kumaliza chuo Upendo alipata rafiki wa kiume aliyeitwa James ambaye alikuwa ni mfanyabiashara. James naye alisoma Chuo Kikuu cha Dar es Salaam siku za nyuma lakini aliamua kufanya kazi zake binafsi kutokana na ajira kuwa ngumu. Kadiri siku zilivyozidi kwenda urafiki wa James na Upendo ulikua na kuimarika sana kiasi kwamba watu waliokuwa wakiwaona pamoja walijua ni mke na mume.

Siku moja James akiwa amekaa nyumbani kwake maeneo ya Kinondoni aligubikwa na wazo zito kuhusu Upendo.

“Mimi na Upendo ni marafiki wakubwa sana na huyu binti ni msichana ambaye anajiheshimu sana tokea nilipomfahamu, nimempenda sana kutoka moyoni mwangu natamani awe mama wa watoto wangu. Kwa vile sijawahi kumtamkia lolote juu ya suala la mapenzi kwa kipindi chote cha kufahamiana kwetu, nahisi nikimdokeza tu pengine anaweza akachukia.”

Aliwaza James huku akitamani kumwambia Upendo kuhusu alilonalo moyoni mwake.

Zilipita siku kadhaa kila James akionana na Upendo akawa anataka kumwambia lakini alikuwa anasita. Siku moja alipanga kumtoa Upendo ili kwenda naye sehemu tulivu apate fursa nzuri na adimu ya kumwambia Upendo juu ya mapenzi aliyonayo moyoni mwake.

Ilikuwa siku ya Ijumaa James aliyopanga kumtoa Upendo jioni yake kwenda katika matembezi. Alipomweleza Upendo juu ya azima yake ya kutoka naye alikubali bila pingamizi. Ilipofika jioni ya saa kumi na mbili hivi James alikwenda Hosteli ya Mabibo na gari yake aina ya Benzi kumchukua Upendo. Alipofika Hosteli block A chumba namba 228 alimkuta Upendo akiwa tayari amejitayarisha kwa ajili ya matembezi ya jioni. Upendo alivalia vazi la kutokea jioni ambalo lilimkaa barabara

likionyesha vizuri jinsi Mungu alivyompendelea kimaumbile. Alipendeza sana kiasi kwamba James alijiona ni mwanamume mwenye bahati kama angefanikiwa kumpata kimapenzi.

James aliendesha gari kuelekea Sinza eneo liitwalo Madukani katika Mgahawa uitwao “Fast Food and Take Away” ambao ulikuwa na utulivu na hali ya hewa nzuri. Walichagua sehemu nzuri na kwenda kukaa pamoja.

James alimpa Upendo uhuru wa kuagiza chochote alichopenda kula na kunywa. Waliletewa vinywaji na kuanza kunywa huku wakisubiri chakula.

Muda wote mapigo ya moyo wa James yalikwenda mbio akiwaza namna ya kuanza kumwambia Upendo suala la mapenzi. Baada ya kama dakika ishirini hivi za maongezi ya kawaida James aliamua kumwaga sera zake.

“Upendo umependeza sana leo hilo gauni ulilovaa limekupendeza sana.” James alianza kwa kumsifia Upendo.

“Asante James mbona hata wewe umependeza.” Wote wakacheka na kugonganisha mikono.

James alivuta kiti chake na kusogea karibu na Upendo huku moyo wake ukiwa bado unamdunda macho yakiwa na rangi nyekundu kwa hofu ya kumwambia Upendo kuwa anampenda. James alijikaza na kumshika Upendo mkono.

“Upendo kuna kitu kinanisumbua sana moyoni mwangu, kitu hicho kimekuwa kinanitesa kwa muda mrefu sana tangu tufahamiane.” Aliongea James huku midomo ikimtetemeka kidogo.

“James! Ni kitu gani hicho jamani?” Aliuliza Upendo kwa sauti ya mahaba na macho yake ya kurembua.

“Ni kitu cha kawaida sana lakini…”

“Lakini nini?” Alimkatisha Upendo akiwa ananyanyua glasi ya soda na kuinywa huku akimwangalia James usoni.

“Nitakwambia kitu hicho jioni hii ya leo ingawa kitu hicho kinaweza kuharibu au kuboresha urafiki wetu.” Aliongea James kwa kujihami ili apate ujasiri wa kusema.

“We sema tu James, ni jambo gani hilo ambalo unasita kuniambia wakati kuna mambo mengi sana tumekwishaongea mimi na wewe tangia tufahamiane.” Upendo aliongea kana kwamba anampa uhuru wa kusema linalomsumbua James.

“Upendo! Aliita James kwa sauti ya chini sana huku akijitahidi kuyakwepa macho ya Upendo.

Abee!” Aliitikia Upendo.

“Ahhm! Tangu tufahamiane nimetokea kukupenda zaidi ya urafiki tulionao.” James alitulia kidogo huku safari hii akimwangalia Upendo usoni. Kabla Upendo hajasema kitu James aliendelea kumwaga sera zake huku Upendo akiwa kimya.

“Ningependa uwe mpenzi wangu na baadaye Mungu akitujalia uwe mama wa watoto wangu.” Aliongea James akimkazia macho Upendo.

Upendo aliyekuwa ametulia akimsikiliza aliutoa mkono wake mikononi mwa James ambaye alikuwa amemshika, huku akiinama na kuminyaminya vidole vyake kwa aibu.

“Mh! We James! Ina maana hadi sasa hauna mwanamke kijana mzuri kama wewe acha hizo bwana mbona si kitu cha kawaida.” Alihoji Upendo.

Ni kweli Upendo lazima utafikiria hivyo, ila nakwambia ukweli kutoka moyoni mwangu, sina mwanamke yeyote. Ila niliwahi kuwa na mpenzi zamani kidogo tukakorofishana na kwa sasa ameolewa. Nilikuwa nampenda sana ila aliniumiza moyo wangu nikajikuta sitamani kuwa na mwanamke tena maishani mwangu. Lakini tulipoanza urafiki mimi na wewe nimegundua kuwa nahitaji kuyaanza maisha yangu upya.

Nimekupenda sana Upendo nipe nafasi katika moyo wako.” Alibembeleza James.

“Je, kwa sasa huyo aliyekuwa mpenzi wako anaishi wapi?” Aliuliza Upendo.

Alikuwa anaishi hapahapa Dar lakini baada ya kuolewa alihamia Mbeya

na mume wake.

“Mmmh!! Hapana James kwa sasa, naona tuendelee kuwa marafiki, ila nitakujibu kuhusu ombi lako siku yoyote.” Alimjibu Upendo hukuakitafakari kitu.



“Nikupe muda gani Upendo.” Alihoji James huku akishusha pumzi kwa nguvu. Kisha akaendelea kuongea.

“Nashindwa hata kusubiri. Ila sawa nitakupa muda ili uweze kunifikiria, fahamu kuwa nakupenda na ni wewe pekee unaye utesa moyo wangu kwa sasa. Natumaini nitapata jibu zuri. Au siyo?” Aliuliza James huku akitabasamu na kuweka mkono wake wa kulia begani kwa Upendo.

“Jamani mbona una haraka hivyo usijali tutaona itakavyokuwa.” Alijibu

Upendo huku akitabasamu kama alivyofanya James lakini akiuondoa

mkono wa James uliokuwa juu ya bega lake.

Baada ya hapo chakula kilikuwa tayari kimeletwa, walikula na kuendelea

kunywa vinywaji vyao na kuzungumza mambo mbalimbali. Ilikuwa tayari

imetimia saa tatu za usiku.

“Heh! Kumbe muda umeenda hivi hebu nirudishe hostel James, nina kazi za chuo sijazimaliza.” Alitamka Upendo.

“Acha hizo Upendo yaani saa tatu tu ndo muda umeenda. Mimi ningependa twende na disko lakini kwa vile umesema kuwa una kazi za kufanya, sina namna ngoja tu nikupeleke. Ila tumalizie vinywaji kwanza.” Alishauri James.

Baada ya kumalizia vinywaji waliondoka kuelekea hosteli. Wakiwa njiani,

James aliendelea kubembeleza na kusisitiza juu ya ombi lake.

“Please (nakuomba) usiache kunifikiria nakupenda sana Upendo.” Alisisitiza James.

Upendo alinyamaza kimya huku akimwangalia James bila kumjibu chochote. Walipofika hosteli kabla hajashuka katika gari James alimshika mikono yote miwili kisha akamkumbatia na kumbusu shavuni.

“Nakupenda sana Upendo. Nakutakia usiku mwema na ndoto njema.”

Aliongea James wakati akiendelea kumbusu huku Upendo akijaribu

kumzuia.

Mapigo ya moyo yalimwenda mbio Upendo, huku akijitoa kifuani kwa

James.

“James asante kwa yote nakutakia usiku mwema nawe.” Alishukuru

Upendo kisha akashuka kwenye gari na kuingia hosteli huku James

akiondoka kuelekea Kinondoni.

Usiku kucha Upendo aliwaza sana akimwaza James moyoni mwake.

“Mmh! Mmh! James ni kijana mtanashati siwezi kumpoteza nampenda

pia. Lakini wanaume nao hawatabiriki, leo ananibembeleza sana akidai

kuwa ananipenda halafu akinipata ataniacha. Ikitokea hivyo ataniumiza

moyo wangu sana. Mmh! lakini sidhani kama James atakuwa hivyo,

natamani awe baba wa watoto wangu. Sijui nimpigie simu ni mwambie

sasa hivi! Lakini hapana! Aa! Hebu ngoja nimpigie sasa hivi.” Alichukua

simu yake na kuanza kumpigia simu James,

Wakati simu ikiwa inaita Upendo alikuwa na hofu kubwa.

“Haloooo! Alipokea simu James.

“Yaani nilitaka kukupigia simu muda huu umeniwahi, niambie mpenzi

wangu.” Aliongeza James bila kumpa nafasi upendo ya kuongea.

“Aha vipi James uko wapi? Unafanya nini saa hizi? Unajua kuna kitu

nataka nikwambie ila basi, nitakwambia kesho, usiku mwema.” Akakata

simu Upendo.

“Aah! Kakata simu.” Aliwaza James kisha akaamua kupiga yeye.

“Halooo! Mbona umekata simu kabla hatujamaliza maongezi? Aliuliza

James

“Haya niambie ulichotaka kuniambia kwani natamani sana kusikia kutoka

kwako la sivyo utanifanya nisilale.” Aliomba James.

“Hakuna kitu jamani James nilikuwa nataka kujua kama umefika salama.”

Alijibu Upendo.

Usiku ule Upendo hakumwambia chochote James akabaki akijilaumu

baada ya kukata simu huku akiwaza;

“Hivi kweli nimeshindwa kumjibu! Ila kesho tukionana nitamwambia.”

Upendo aliendelea kumwaza James hata kusoma kulimshinda usiku ule

akaamua kulala.

Kesho yake ilikuwa ni siku ya Jumamosi, asubuhi Upendo aliingia darasani

kujisomea kama kawaida yake. Ilipofika saa sita na nusu aliamua kurudi

hosteli. Akiwa chumbani na rafiki yake Grace aliamua kutoka nje ili apate

muda mzuri wa kutafakari kuhusu ombi la James. Alimuaga Grace na

kumwambia kuwa atakuwa chini ya mti mkubwa ulio nyuma ya hosteli

akijipumzisha.

Baadaye James alikuja pale chumbani kwa Upendo bila taarifa, baada ya

kugonga mlango na kuruhusiwa kuingia alimkuta Grace akiwa amejilaza kitandani akisoma gazeti.

“Habari gani dada!” Alisalimia James.

“Nzuri kaka karibu kiti.” Alijibu Grace.

“Asante dada. Aaahmm! Nimemkuta Upendo?” Aliuliza James huku

akitabasamu.

“Ndiyo! Ila yupo nje amekaa chini ya mti mkubwa nyuma ya jengo hili.”

Alijibu Grace huku akiamka na kukaa vizuri kitandani.

“Haya asante hebu nimfuate.” Aliaga James na kuondoka.

Upendo alikuwa amekaa kwenye kiti cha plastiki huku amegeukia uzio

unaozunguka hosteli akichezea tawi dogo la mti. Mara James alikuja

kimyakimya akitokea kwa nyuma na kumziba Upendo usoni bila ya yeye

kumwona akiwa amebeba chakula kwenye mfuko. Upendo alishtuka sana

katu asijue ni nani aliyemziba macho.

“Nani tena jamani? Mimi huwa sipendi michezo ya hivi.” Alilalamika

Upendo.

“Usiogope Upendo ni mimi.” James alitoa mikono yake na kumbusu

Upendo.

“Waoo! James mbona hukunipigia simu kunitaarifu kama unakuja?”

Aliuliza Upendo huku akisimama kupokea mfuko aliokuwa ameubeba

James.

“Nimekuletea chakula cha mchana Upendo.” Alitamka James bila kujibu

swali aliloulizwa.

“Mmh! Nilijua ni watu wameamua kunichokoza. Asante sana kwa

kuniletea chakula, umejuaje James kwani mpaka saa hizi sijala njaa

inaniuma kweli. Ehee! umeniletea chakula gani?” Aliuliza Upendo.

“Fungua uone.” Alijibu James.

“Ooh! Chipsi na kuku napenda sana chakula cha aina hii, vipi njoo basi

tule wote.” Aliongea Upendo kwa shauku huku akimalizia kufungua

mfuko.

Upendo alichukua maji ya chupa aliyokuwa nayo na kumwomba James

anawe mikono ili wale wote.

“Hapana mimi nimeshakula we kula tu usijali nimekuletea wewe.” Alijibu

James huku akipokea chupa ya maji ili kumnawisha Upendo.

Akiwa anaendelea kula Upendo alikuwa ana mawazo mengi sana juu ya

James.

“Upendo napenda sana uwe mke wangu, kwa nini unaamua kuutesa moyo

wangu hivi?” Aliuliza James huku akimwangalia Upendo kwa kumtamani.

“Kwanini unasema nakutesa James nataka tu kuwa na uhakika kwani

naogopa sana kudanganywa.” Alijibu Upendo huku akimwangalia James

kwa kurembua macho.

“Niamini Upendo, mimi kamwe siwezi kukudanganya nakupenda kutoka

moyoni mwangu.” Alijibu James huku akimkazia macho upendo.

“Kweli James? Hata mimi nakupenda sana James ila...” Alisita Upendo.

“Ila nini.” Aliuliza James huku akiweka mkono wake begani kwa Upendo.

“Ngoja nije.” Aliinuka Upendo kuekelea chumbani kwake akimwacha

James akishangaa kulikoni.

Baada ya dakika kama tano, Upendo alirudi akiwa ameshika bahasha

mkononi iliyoandikwa “JAMES” ambayo aliiandika usiku ule, ili

wakionana ampe. James alimwangalia Upendo kwa mshangao asijue

chochote.

“James! Nimefikiria sana kuhusu ombi lako, nikatamani kukujibu usiku

kwenye simu, lakini ulimi ulinikwama nikashindwa kuongea. Hivyo majibu

ya ombi lako yako humu.” Alimaliza kuongea Upendo huku akimkabidhi

James ile bahasha.

James alipokea ile bahasha huku mkono ukitetemeka kidogo na

kumwangalia Upendo usoni ambaye aliukwepesha uso wake na kuangalia

pembeni kwa aibu. Kisha akaamua kuifungua bahasha na kusoma

yaliyokuwemo ndani kwa makini huku akiinuka kumwangalia Upendo,

ambaye sasa alikuwa amefunika uso wake kwa viganja vyake vya mkono.

Haya ndiyo maneno aliyoyakuta James:

Mapenzi ni matamu kama asali wawili tukipendana.

Mapenzi ni machungu wawili tukisalitiana.

Mapenzi ni zawadi daima tukipendana.

Mapenzi ni lulu dhati tukipendana.

Mapenzi ni kufa na kuzikana.

Nakupenda

Uwe Baba!

Watoto!

Wangu!

Baada ya kumaliza kusoma ile karatasi James alimwendea Upendo na

kumnyanyua kisha akamkumbatia huku naye Upendo akizungusha

mikono yake na kumkumbatia James kwa nguvu kiunoni.

“Nashukuru sana mpenzi nakuahidi wewe ndio mke wangu.” Aliongea

James huku akiendelea kumrushia mabusu motomoto, huku naye Upendo

akijibu kwa kumbusu James ikiwa ni ishara ya kufungua ukurasa mpya wa

uhusiano wa James na Upendo.



************* Baada ya miezi sita ********************



Baada ya mapenzi kukolea James aliamua kumtambulisha Upendo kwa

wazazi wake. Baba na mama wa James walimpenda sana na kuwashauri

wafunge ndoa pindi tu Upendo akimaliza Chuo. Upendo alikuwa ndo

anaingia mwaka wa mwisho ili ahitimu katika shahada ya Sheria. Kadiri

siku zilivyozidi kusonga mbele James na Upendo waliyafurahia sana

mapenzi yao. Ili kuimarisha zaidi uhusiano wao James alimwomba

Upendo waende kwa wazazi wake ili kutambulisha rasmi. Basi walipanga

safari ya kwenda Morogoro ambako walipokelewa vizuri sana na wazazi

wa Upendo. Baadaye wazazi wa Upendo waliwaasa juu ya uhusiano wao

kuwa usiathiri masomo ya Upendo. Wazazi wake Upendo walishauri

kwamba Upendo amalize Chuo kwanza na atafute kazi ndipo wafikirie

suala la kufunga pingu za maisha.

Wakati James akiwa Morogoro mdogo wake Upendo alikuwa chuoni.

Baada ya kukaa siku kadhaa Morogoro James na Upendo walirudi Dar es

Salaam. Kutokana na ushauri wa wazazi wa pande zote mbili maisha ya

James na Upendo yalikuwa ni ya furaha siku zote yenye mategemeo

mazuri katika kuleta maendeleo ya maisha yao ya baadaye.





Akiwa chuoni Upendo alisoma kwa bidii sana na James aliendelea na

biashara zake. Siku moja Upendo alimpigia simu mdogo wake na

kumwambia juu ya uhusiano wake na James.

“Haloo! Mambo mdogo wangu! Mzima wewe! Habari za Chuo?” Ilikuwa

ni sauti ya Upendo katika simu.

“Nzuri ndugu yangu mambo magumu sana chuoni, bora wewe

mwenzangu unakaribia kumaliza.” Alisema Eliza.

“We! Hakuna cha uafadhali wowote na hiyo mitihani inavyokuja migumu

nimetingwa ile mbaya. Kumbuka wewe si ulisema ukienda chuo utajirusha

sana. vipi imekuaje.” Aliuliza Upendo.

“Yaani, we acha tu ‘my sister’ (dada yangu) sina hata huo muda wa kujirusha

nikicheza mbona nitafeli mmh nipe umbea maisha vipi.” Alihoji Eliza.

“We nawe kwa umbea, Eliza mwenzio nimepata mchumba nikimaliza

Chuo naolewa.” Alisema Upendo huku akicheka.

“Usiniambie! Hongera mwaya, haya huyo shemeji anafanya kazi gani?”

Aliuliza Eliza.

“Ni mfanyabiashara na pia huwa anakuja Arusha mara kwa mara, nadhani

mtaonana au ukija likizo utamwona. Nyumbani nilishampeleka

kumtambulisha kwa wazazi.” Alieleza na kufafanua Upendo.“

“He! Kumbe mmefika mbali hivyo hata kuniambia mwenzio.” Alilalamika

na kulaumu Eliza.

Eliza huku akiwa na shauku ya kutaka kumfahamu shemeji yake, Upendo

akajitetea;

“Wala sio hivyo ‘my young sister’ (mdogo wangu) mambo yalikwenda

harakaharaka lakini, utamfahamu na wewe ndiye utakuwa mstari wa mbele

kwenye harusi yangu.” Aliongea Upendo kwa majivuno.

“Haya bwana mimi nakutakia mafanikio mema Mungu awajalie mfikie

malengo yenu.” Alisema Eliza basi wakaendelea kuzungumza na baadaye

walikata simu na kuendelea na mambo mengine.

Kutokana na kazi kuwa nyingi za kusafiri mara kwa mara James alipata

safari ya kwenda Arusha kikazi. Wakati huo ilikuwa ni kipindi cha mitihani

kwa Upendo basi, waliagana. Siku hiyo walikuwa pamoja ikiwa ni siku

moja kabla ya James kuondoka .

“Mpenzi wangu, utanikosea sana ukichelewa kurudi si unajua

nimekuzoea.” Aliongea Upendo kwa sauti ya mahaba.

“Usijali mpenzi ni kazi zinanifanya nisafiri nitawahi kurudi ila na wewe si

una mitihani kwa sasa inabidi usome kwa bidii ili ufaulu vizuri sawa

mama?” Aliongea James huku akimsogeza Upendo kifuani mwake na

kumkumbatia.

“Sawa lakini si unajua sipendi kukukosa siyo uende huko ukanisahau

kwa kujirusha na vimwana vya Arusha.” Upendo alisisitiza.

“Ina maana huniamini mamii nakupenda sana hakuna mwanamke wa

kunidanganya wala usijali.” Alijibu James huku akitabasamu.

Walizungumza sana siku ile wakiwa nyumbani kwa James na baadaye

walikwenda kupumzika.

Kesho yake mapema saa mbili asubuhi James aliondoka na huku

akisindikizwa na mpenzi wake hadi uwanja wa ndege tayari kwa kuanza

safari. Baadaye Upendo alirudi chuoni kuendelea na masomo. Alipofika

Arusha James alikwenda moja kwa moja hadi katika hoteli ya Ngurdoto

yenye mandhari nzuri sana. Alipata chumba na baada ya kuingia kwenye

chumba chake alimpigia simu mpenzi wake kumtaarifu kuwa amefika

salama.

“Mambo mpenzi wangu! Nimefika salama nipo Hoteli ya Ngurdoto

natamani tungekuwa pamoja,” Aliongea James kutoka Arusha.

“Hata mimi pia natamani tungekuwa pamoja mpenzi, ila majukumu ndiyo

yanatubana. Hapa nilipo najisomea yaani hii mitihani inayokuja inaniumiza

kichwa sana.” Aliongea Upendo kwa unyenyekevu.

Nakuomba usinisaliti mpenzi, najua kuna wanaume wengi

wanakufuatafuata. Ziba masikio yako usisikie neno lolote kutoka kwa

mwanamume yeyote. Alitahadharisha James.

“Mmh we nawe kwa wivu, nakupenda sana siwezi kufanya hivyo hata

siku moja.” Alijibu Upendo.

Baada ya mazungumzo kila mmoja aliendelea na mambo yake.

Akiwa Arusha James alianza kufanya kazi zilizompeleka akiwa na marafiki

zake ambao ni wenyeji wa huko walizunguka sehemu mbalimbali ikiwa ni

wiki mbili tangu James aondoke Dar es Salaam. Siku hiyo ilikuwa ni siku

ya Ijumaa muda wa saa mbili usiku ambapo James na marafiki zake

walikwenda katika matembezi maeneo ya Sakina.

Walipofika huko walikunywa sana pombe huku wakiwa wanafurahi

pamoja wakati huo walikuwa Sakina Bar, waliendelea kunywa hadi ilipofika

saa tano usiku.

“Aisee washikaji kwa nini tusiende disko Triple A.” James aliyekuwa

ameshalewa aliwashauri wenzake.

“Swadakta! Hilo neno! Washikaji twendeni disko sijaenda siku nyingi sana

nadhani itakuwa safi sana.” Mmoja wao aliongea huku akionyesha ishara

ya kuondoka.

Walikubaliana na kuanza safari ya kwenda ukumbi wa Disko wa Triple A

ambao haukuwa mbali sana na mahali walipokuwa. Kabla ya kupanda gari

waliokuwa nalo James alichukua simu yake na kumpigia Upendo.

“Haloo mamii vipi umelala mamaaa!” Aliongea James.

“Safi mpenzi wangu nilale kwa raha gani niliyonayo? Hapa nilipo nipo

bize sana na maandalizi ya mitihani. Vipi uko wapi mbona nasikia kelele?”

Alijibu na kuuliza Upendo.

“Nipo na washikaji tunafurahi mpenzi wangu. Mimi nakutakia usiku

mwema.” Alijibu James ambaye hakusema kama alikuwa anaelekea disko.

“Vipi James yaani huyo mwanamke amekubana mpaka umwambie

unakwenda wapi? Kweli ninyi ndiyo wale hata ukitaka kula utampigia simu

na kumwambia unachokula. Aaa! hebu twendeni alishauri Rama mmoja

wa rafiki zake wapendwa wa James.

“Acha hizo Rama huyu mama watoto wangu na kuhusu disko

sijamwambia kwani ingekuwa balaa muda huu”. Alijibu James huku

akitabasamu.

Walipofika disko walikaa na kuendelea kunywa sana. Huko disko kulikuwa

na watu wengi wakiwemo wasichana warembo sana ambao James na

marafiki zake walianza kutafuta wasichana wa kucheza nao. James

alisimama na kumfuata dada mmoja aliyekuwa amekaa karibu naye na

kumuomba wacheze. Yule dada alikubali na kusimama na kuanza kucheza

naye. Kama kawaida, katika kucheza kuna mambo mengi, wakiwa

wanacheza James alimshika yule dada mkono na kumsogeza pembeni

sehemu iliyokuwa haina kelele na kufanya mazungumzo naye.

“Mrembo umependeza sana, halafu unajua kucheza sijui unaitwa nani.”

Aliuliza James huku akimwangalia kwa makini yule dada usoni.

”Asante kaka mimi naitwa Esta.” Alijibu yule msichana huku akitabasamu

na kurembua macho.

“Una jina zuri sana Esta kama ulivyo mwenyewe.” Alisema James huku

akimtazama Esta ambaye alikuwa akitabasamu.

“Mbona wewe hujaniambia jina lako.” Aliuliza yule msichana.

“Usijali mrembo mimi naitwa Juliasi.” Alijibu James.

Basi wakafahamiana na kuendelea kucheza pamoja baadaye James

alimwomba Esta waondoke pamoja naye Esta alikubali na kuondoka huku

akiwaacha marafiki zake bila hata ya kuwaaga. Walichukua teksi nje na

kuelekea katika hotelini, wakiwa njiani walikuwa wamekumbatiana kila

mmoja akimwambia mwenzake maneno ya kimahaba hadi walipofika

hotelini na kuingia chumbani. Wakiwa ndani James alikuwa amechoka sana

kutokana na pombe alizokunywa. Lakini Esta yeye alikuwa amelewa

kidogo hivyo alimsogelea James na kumvua shati taratibu pamoja na

suruali yake kisha kumwacha akiwa katika bukta. Baada ya kumaliza

kumvua kila kitu alimpandisha kitandani James akawa ametulia kimya

kama vile amemwagiwa maji.

Naye Esta alivua nguo zake na kuziweka pembeni na kisha akamsogelea

James.

“Juliusi we ni mwanamume mzuri sana nafurahi kuwa pamoja na wewe

haijawahi kunitokea nikamwamini mwanaume kwa haraka kama ilivyo

kwako nimekupenda naomba usiniache.” Esta aliizungumza maneno huku

akiwa anamshika katika paji la uso naye James taratibu alinyanyuka na

kuanza kumbusu Esta bila hata ya kuzungumza lolote huku akimkumbatia

na baadaye walilala usingizi wa pono.

Ilipofika asubuhi Esta aliamka na kwenda kuoga wakati James alikuwa

bado amelala usingizi mzito. Baada ya Esta kutoka bafuni alikaa katika

sofa lililokuwa pale chumbani huku akiwa anamsubiri James aamke.

“Mmh sijawahi kupenda kiasi hiki huyu mwanamume sijamfahamu vizuri ni siku moja tu lakini nimempenda sana naamini atakuwa ni mwanamume wa maisha yangu.” Aliwaza Esta huku akimwangalia James.

Wakati akiwa anaendelea kuwaza mara ghafla James aliamka kutoka usingizini na kukaa pale kitandani huku akionekana kuchoka sana.

“Habari za asubuhi Juliasi mpenzi wangu umelala sana”. Esta alimsalimia

James.

“Jana nilikuwa nimekunywa pombe nyingi sana vipi unaweza ukaondoka

tu muda huu usijali mimi nipo sawa tu.” Alijibu James.

“Sawa mpenzi mimi nitaondoka kwani hata hivyo nilikuwa na kazi ya

muhimu naifuatilia ila naamini usiku tutakuwa pamoja nataka tuzungumze zaidi.” Esta alisema huku akiwa ananyanyuka na kumsogelea James kisha kumbusu na kuchukua mkoba wake kuondoka kwa furaha sana. James alichukua waleti yake na kutoa kiasi cha shilingi laki moja na kumkabidhi

Esta.

“Nimefanya nini mimi nimemsaliti mpenzi wangu Upendo itabidi niwe makini sana hiki kitu asikifahamu vinginevyo itakuwa balaa.” Aliwaza

James baada tu ya Esta kuondoka.

Basi James alinyanyuka na kwenda kuoga na baadaye aliendelea na kazi zake kama kawaida. Ilipofika jioni Esta alimpigia simu James na kutaka

kuonana naye. James alimtaka Esta aende hotelini usiku ili waendelee na

huo mchezo huku James akiwa anafanya kwa siri Upendo asijue.

Ilipita kama miezi miwili hivi James akiwa bado yupo Arusha akiwa

anaendelea na shughuli zake na bado akiwa na uhusiano wa kimapenzi

kwa siri na Esta.



*********



******************

Huko Dar es Salaam Upendo alikuwa mpweke sana kwani alikuwa

amemaliza mitihani ila hakwenda Morogoro alibaki Dar es Salaam na

alikuwa akiishi katika nyumba ya James Kinondoni. Wakati wote walikuwa

wakiwasiliana na mpenzi wake vizuri. James alitakiwa kukaa Arusha kwa

muda wa miezi minne ndio shughuli zake zitakuwa zimekamilika, kwa

hiyo alikuwa akimtaka Upendo avumilie na waendelee na mikakati ya

kufunga ndoa ili punde akirudi tu wafunge ndoa.

Upendo aliendelea na mikakati ya harusi huku akishirikiana na wazazi

wake pamoja ili kuandaa sherehe ya kumuaga Upendo. Akiwa katika

mikakati ya harusi alimpigia simu mdogo wake ili kumjulisha mambo

yanavyoendelea.

Simu iliita kwa muda mrefu bila kupokelewa lakini baadaye ilipokelewa.

“He! We Eliza mbona umechelewa kupokea simu?” Aliuliza Upendo.

“Mh dada samahani nilikuwa bafuni, ehe niambie.” Alijibu Eliza.

“Ndugu yangu natamani ungekuja huku unisaidie katika mipango ya

harusi yangu vipi mnafunga lini chuo?” Aliuliza Upendo.

“Makubwa! Kweli mapenzi yamepamba moto ndio unaolewa na huyo

shemeji hata simjui jamani?” Alihamaki Eliza.

“Wewe nawe! Utakuja kumwona siku ikifika. Kwanza yupo huko Arusha

lakini ametingwa sana sijui kama mtaweza kuonana.” Alisema Upendo.

“Hee! Jamani kweli shemeji yangu yupo huku halafu huniambii? Vibaya

hivyo dada yangu, sasa kuhusiana na mimi kuja huko kukusaidia hiyo

mipango yako ya harusi kwa sasa itakuwa vigumu kwani najiandaa na

mitihani itakayoanza mwezi ujao.” Alijibu Eliza.

“Jamani Eliza mwenzio natamani ungekuwepo ila hakuna tatizo kwani

masomo nayo ni muhimu. Mh mdogo wangu hebu niambie sijapata

shemeji mmasai huko?” Aliuliza Upendo huku akicheka.

“Mmh! mwenzangu nimepata mchumba nampenda sana, mambo yakiwa

sawa nitakufahamisha.” Alijibu Eliza.

Basi waliendelea kuzungumza na baadaye kila mmoja aliendelea na

mambo yake.

James kipindi chote akiwa Arusha alikuwa akimsaliti Upendo na kustarehe

na Esta. Baada ya siku kadhaa kupita hatimaye siku za James kurudi Dar

es Salaam zilikaribia. Esta alimfuata James hotelini ili kuzungumza naye

kuhusiana na hatma ya uhusiano wao watakapokuwa mbali.

“Juliasi karibu utaondoka kwenda Dar hivi kweli utanikumbuka? Na jinsi

warembo walivyo wengi huko Dar?” Aliuliza Esta huku akimpapasa uso

James.

“Hapana siwezi kukuacha mpenzi wangu tutawasiliana usijali. Arusha

nitakuja hata wewe utakuwa unakuja Dar es Salaam.” Alijibu James huku

akimbusu Esta katika shavu la upande wa kushoto.

“Sawa hakuna tatizo mimi naomba tuendelee kuwasiliana nakupenda sana

mpenzi wangu.” Alijibu Esta huku akiwa amemkumbatia na kumbusu

James.

******************

Huko Dar es Salaam Upendo alikuwa anaandaa mapokezi ya kumpokea

mchumba wake James ambaye walikuwa hawajaonana yapata miezi minne.

Alifanya usafi wa mazingira ya nyumba na kubadilisha baadhi ya vitu ili

kuonekane tofauti. Alikuwa na furaha sana siku hiyo ambapo kesho yake

James ndiyo alikuwa akirud.i Alinunua maua mazuri ya rangi nyekundu

pamoja na mvinyo.

Kesho yake James alirudi, Upendo alikwenda kumpokea uwanja wa ndege

yapata saa moja jioni. James alishuka kwenye ndege na kuelekea sehemu

za mapokezi na kumkuta Upendo aliyempokea kwa furaha sana.

“Darling (mpenzi) umependeza sana, umezidi kuwa mweupe, nimefurahi

sana kuwa nawe tena” Aliongea James huku akiwa amemkumbatia

Upendo.

“Yaani James nimefurahi sana umerudi nilikuwa mpweke sana.” Alijibu

Upendo huku akimpokea James begi.

Walielekea Kinondoni nyumbani kwa James. James alishangaa sana kuona

mabadiliko ya nyumba yake na jinsi ambavyo Upendo alikuwa amepamba.

“Mpenzi unafaa sana katika mambo ya upambaji nyumba imekuwa tofauti

kabisa nimefurahi kweli wewe ni mke mzuri.” Aliongea James kwa furaha

huku akikaa kwenye sofa.

“Asante mpenzi wangu nenda ukaoge uje tule chakula halafu unipe habari

za Arusha.” Upendo alimsihi James. Usiku ule ulikuwa ni usiku wa furaha

kwa wote wawili walikula na kunywa na kulala huku wakiwa na mikakati

ya kufunga ndoa haraka.

Hatimaye maandalizi ya kumuaga Upendo yalikamilika na wakati huo

wazazi wa James walikuwa wakiandaa harusi. Mawasilianao ya Esta na

James yalipungua sana. Kila Esta akimpigia simu alikuwa akimdanganya

kuwa ametingwa sana, kitu ambacho kilikuwa kikimuumiza sana Esta.

Hata hivvyo Esta aliendelea kujipa moyo kuwa Juliasi anampenda bila

kujua kuwa alikuwa ni tapeli wa mapenzi. Baada ya miezi miwili kupita

Esta aliugua homa na kwenda hospitali ambapo alipimwa na kukutwa

akiwa na ujauzito wa miezi miwili. Kutokana na hali hiyo Esta

alichanganyikiwa sana.

“Mungu wangu nina mimba ya Juliasi nitafanyaje mimi na huyu

mwanamume sijui ana mpango gani na mimi. Nafikiria kuitoa mimba

lakini naogopa sana. Hapana lazima nimfahamishe hali halisi kwa sababu

sijui nifanyeje. Kwani nyumbani baba akijua ataniua na ndugu zangu

watanifikiriaje, nikifika chuo ni lazima nimpigie simu leo.” Aliwaza Esta

huku machozi yakimlengalenga.

Esta aliondoka pale hospitali akiwa na mawazo mengi sana. Alipofika

chuoni aliingia chumbani kwake na kupiga simu. Simu iliita muda mrefu

bila kupokelewa. Aliendelea kupiga kama mara mbili bila mafanikio hadi

alipojaribu tena ndipo simu ilipokelewa na James aliyekuwa kazini kwake

muda huo.

“Haloo vipi Juliasi mbona nakupigia simu yangu hupokei?” Auliza Esta.

“We mwanamke mjinga kweli inamaana niache kazi zangu nipokee simu

yako? Je, hujui kwamba huu ni muda wa kazi? Je, unasemaje?” Aliuliza

James kwa sauti iliyojaa hasira .

“Samahani mpenzi kwa usumbufu nimekupigia nikwambie leo

nimekwenda hospitali kupima nina mimba yako ya miezi miwili.” Esta

alimfahamisha James. “Hee! Nini? Mimba! Ya nani!” Alihamaki James

huku akionyesha kama mtu aliyekanganyikiwa.

“Kweli Juliasi unaweza kuniuliza kuhusu mimba hali unajua ni yako?

Halafu unaniuliza ya nani?” Aliuliza Esta huku amebana pua kumuigiza

James.

“Sikiliza nikwambie Esta, mimi sina mpango wa kuwa na mtoto sasa hivi,

kama wewe ulitaka mtoto ni juu yako ninachoweza kukusaidia ni pesa ya

kutoa hiyo mamba.” Alisema James kwa sauti ya kutetema tofauti na siku

nyingine.

Esta hakuamini maneno anayoambiwa na James”

“Sikujua kama utanifanyia hivi Juliasi, unajua ni kiasi gani nakupenda,

nashukuru sana ila hii mimba sitaitoa na huyu mtoto ni wako na nitamleta

huko huko Dar es Salaam.” Kisha akakata simu na kulia kwa uchungu

huku akijilaumu moyoni mwake na kujipa matumaini”

“Nilijua Juliasi ni mwanaume mkweli kumbe yuko hivi au kwa sababu ya

hii mimba imekuja ghafla, sijui nifanyeje naamini mambo yatakwenda

sawa, ngoja nimwache kwanza kwa sasa.” Alijipa moyo Esta.

Esta aliendelea kuwaza sana na baadaye akamua kuendelea na shughuli

zake za kawaida.

James naye alibaki akiwaza moyoni mwake.

“Hivi nimefanya nini mimi huyu msichana ana mimba yangu na hataki

kuitoa na mimi nafunga ndoa hivi karibuni. Sijui itakuwaje ila ngoja

nimwache siwezi kumpoteza Upendo nampenda sana na ndio mke

wangu, sitaki mawasiliano na huyu mwanamke tena.”

Basi naye aliendelea na mambo yake huku akiwa anajiandaa na harusi

yake. Wakati huo Upendo alipanga safari ya kwenda Morogoro kwani

ilikuwa imebaki kama mwezi mmoja afanyiwe sherehe ya kuagwa na

wazazi wake.

Baada ya wiki kadhaa kupita mawasiliano kati ya James na Esta yalikwisha

kwani kila Esta alipojaribu kupiga simu James alikuwa hapokei. Na

ikitokea amepokea alimtaka asiendelee kumpigia simu tena. Upendo

aliondoka na kwenda Morogoro kwa ajili ya kuandaa sherehe. Akiwa

Morogoro mdogo wake alikuwa bado yupo chuoni, hivyo wazazi wake

walimpigia simu na kumwambia ni lazima awepo kwenye sherehe ya dada

yake.

Zikiwa zimebaki kama wiki mbili kufanyika sherehe ya kumuaga Upendo,

Eliza alirudi Morogoro kwa wazazi wake ili kusherekea pamoja na dada

yake. Siku Eliza alipofika, wazazi wake hawakuwepo ila Upendo pekee.

Upendo alipomwona mdogo wake alifurahi sana, alimpokea begi wote

wakaingia ndani.

“Jamani hatujaonana siku nyingi sana my young sister (mdogo wangu)

mbona umenenepa hivyo ulikuwa unasoma kweli wewe?” Alisema

Upendo.

Eliza alimwangalia sana dada yake:

“Dada Upendo kuna kitu nataka nikwambie, ila iwe siri yako sitaki mama

wala baba wafahamu hili.“ Aliongea Eliza kwa kusihi.

Upendo alishtuka na kuwaza moyoni mwake: “Je, atakuwa ana tatizo

gani?”Aliwaza Upendo. Hebu niambie tafadhali.

“Upendo mwenzio nina mimba hapa nilipo ndio maana unaniona

nimenenepa.” Alianza kueleza Eliza.

“Acha utani wako wewe una mimba ya nani.” Upendo alihoji kwa

mshangao.

“Nina mimba ya kijana mmoja anaitwa Juliasi sijui hata nitampatia wapi

najua anakaa Dar es Salaam, lakini sijui nitaanzia wapi kumpata.” Alisema

Eliza huku akiwa ameinama.

“Inamaana wewe umepata mimba ya mtu ambaye hata ha umjui vizuri,

kweli mdogo wangu umechezea maisha yako.” Aliongea Upendo kwa

kejeli.

Eliza machozi yakiwa yanamtoka,

“Nisaidie dada yangu mimi sijui nifanyeje hapa nilipo kwani hata

mwanamume mwenyewe nikimpigia simu hapokei na ameshakataa hii

mimba ameniambia niitoe na mimi siwezi kufanya hivyo”.

“Haiwezekani! Hiyo mimba usitoe kumbuka nilikuonya mdogo wangu

uwe makini na hawa wanaume. Wengi wao ni matapeli sasaa… ngoja,

tutajua cha kufanya kesho lakini usijali sana kwani tayari jambo limetokea,

kulia siyo sulihisho.” Aliendelea kumbembeleza na baadaye alimtaka

akaoge ajiandae kwani wazazi wao wangerudi muda huo.

Wazazi wao walikuwa wamekwenda kuwachukua ndugu wengine, lakini

walikuwa wanafahamu kuwa Eliza anakuja siku hiyo. Baada ya dakika

kadhaa kupita wakiwa wanaendelea na mazungumzo Baba na Mama yao

pamoja na ndugu wengine walifika. Upendo aliwakaribisha wageni, na

kuwaelekeza sehemu za kukaa.

“Karibuni sana, wengine wakae pale na wengine hapa, waswahili husema

‘sherehe ni watu’, na watu wenyewe ni ninyi, sisi na wengine watakao kuja.”

Upendo aliwaelekeza wageni. Baba Upendo (Mzee George) alimtuma

Upendo akamwite mdogo wake aje awasalimie wageni. Upendo aliinuka

haraka na kuelekea chumbani.

“Eliza unaitwa na baba ili ukawasalimie baba, mama na wageni.

Nakuomba uvae gauni kubwa ili wasielewe mabadilko uliyonayo, kwani

mimba uliyokuwa nayo imeanza kujionyesha.” Alishauri Upendo.

Eliza alijiandaa kama alivyoshauriwa na Upendo kisha wote wakaelekea

sebuleni. Alipofika aliwasalimia wazazi na shangazi yake na wageni

wengnie waliokuwepo

”Jamani ni wewe wajina wangu Esta umekuwa mkubwa hivi”. Shangazi

yake alishangaa kuona Eliza amekuwa mkubwa.

“Yaani dada, hilo jina la Esta mwenzio halitumii anatumia jina la Eliza,

wamekuwa wakubwa sana. Hata sisi hatujawaona siku nyingi. Huyu yupo

chuoni Arusha anaingia mwaka wa mwisho.“ Alifafanua Baba Upendo

huku akimwangalia shangazi yake Eliza na kucheka.

“Kweli siku zinakimbia na hilo jina la Esta ha ulitumii unapenda kuitwa

Eliza mama jamani watoto wa siku hizi.” Aliendelea kushangaa na kucheka

shangazi yake Eliza.

“Hapana shangazi, huwa nalitumia mara moja moja.” Alijibu Esta huku

akiinamisha kichwa chini kwa aibu.

“Lakini bora usilitumie kwani haya majina ya kurithi wakati mwingine sio

mazuri unaweza ukampa mtoto jina la mtu mwenye mikosi na mtoto

akajikuta anakuwa na mikosi katika maisha kwa sababu ya majina ya

kurithi.” Alisema shangazi yake huku watu wote wakiangua vicheko.

“Hakuna wifi hizo ni imani tu za watu.” Alijibu mama Upendo huku

akiinuka kuelekea jikoni.

“Haya jamani huku jikoni vipi?” Aliuliza mama Upendo.

“Tayari mama hakuna tatizo.” Alijibu Upendo.

Waliendelea na mazungumzo pale sebuleni na baadaye baada ya kupata

chakula cha usiku wote walikwenda kupumzika. Hatimaye siku ya sherehe

ilifika, sherehe, iliandaliwa pale nyumbani kwa kina Upendo. Kulikuwa na

uwanja mkubwa ambao ulipambwa vizuri sana. Ama kweli ilikuwa ni siku

ya furaha kwa Upendo.

Kwa upande wa mdogo wake Eliza mambo hayakuwa mazuri kwani muda

wote alikuwa akiwaza sana kuhusu Juliasi kwa nini hapokei simu yake.

“Eliza hii ni siku ya furaha ya maisha yangu naomba uwe na furaha

mdogo wangu. Halafu leo pia ni siku mwafaka kwa wewe kumwona

shemeji yako ambaye hujawahi kumwona, nadhani utampenda kwani

nampenda sana.” Upendo alimfariji mdogo wake huku akimpigapiga

mgongoni na kiganja cha mkono wake wa kulia.

“Nitafurahi sana kumfahamu shemeji yangu nadhani alikuwa akinisikia

tu.” Kwa tabasamu la upole Eliza alimjibu dada yake.“

“Ndiyo nilikuwa nikimsimulia sana kuhusu wewe mdogo wangu kwamba

upo chuoni kwa hivyo leo mtafahamiana au siyo mdogo wangu.” Alisema

Upendo.

“Asante nitashukuru sana kumwona shemeji, sijui atavaa suti, jinsi na

tisheti au atakuwa katika pamba za namna gani.” Aliongea Eliza huku

akitabasanu na kumwangalia dada yake Upendo.

Mipango iliendelea na hatimaye sherehe ilikaribia kuanza. James na wazazi

wake walitokea hotelini na kuelekea nyumbani kwa akina Upendo maeneo

ya Kihonda ambapo sherehe ilikuwa ikifanyika. Walipofika walipokelewa

kwa vigelegele na shangwe nyingi walipelekwa sehemu ya kukaa na

baadaye James alifichwa katika umati wa watu ili Upendo aje kumtafuta.

Upendo alitoka ndani huku matarumbeta yakipigwa na shangwe nyingi

zikitawala akiwa sambamba na mdogo wake Eliza.

Upendo akiwa sambasamba na Eliza alielekea sehemu ile kwenye umati

wa watu ambako James alifichwa ili akamfichue. James akiwa katikati ya

umati alimwona Upendo akiwa anatoka na pembeni akiwa na Esta

alishtuka sana kumwona Esta.

“Mungu wangu yule si Esta? Anafanya nini hapa na mbona yupo karibu

na Upendo? Kuna nini kinaendelea hapa?” James aliwaza na kujiuliza

maswali mengi yaliyokosa majibu.

Kwa muda wa takribani dakika mbili hivi James alikuwa kama mtu

aliyechanganyikiwa. Watu waliendelea kushangilia huku James akiwa hajui

nini cha kufanya baada ya kumwona Eliza ambaye ndio Esta akiwa

anatazama huku na kule kama vile mtu anayetafuta njia ya kutokea.

James akiwa anahangaika nini cha kufanya Upendo na Eliza waliendelea

kuangalia huku na kule wakimtafuta katika umati wa watu. Ghafla Eliza

akamwona Julias na kushtuka, lakini hakujua kama ndio mume mtarajiwa

wa dada yake.

“Haa! Hivi yule si Juliasi? Amefuata nini hapa? Au ni ndugu wa huyo

James? Mmh! Nina bahati kweli sikutarajia kumwona. Sasa hii ni nafasi

nzuri ya kuzungumza naye kuhusu hatima ya uhusiano wetu na hii mimba

yake.” Eliza alijiuliza maswali mengi huku akishangaa na kufurahi kuonana

tena na Juliasi. Zoezi la kumfichua James halikufanikiwa kwani Upendo

alishindwa kabisa kumwona James alipokuwa. Hivyo waliamua kurudi na

kukaa katika sehemu maalumu iliyotayarishwa kwa ajili ya Upendo.

Sherehe ilianza rasmi, watu walijaa sana kushuhudia tukio muhimu la

kuagwa kwa Upendo. Mshereheshaji (MC) aliimudu barabara kazi yake

kwani alifanikiwa kumchangamsha na kumchekesha kila aliyehudhuria.

“Ndugu wageni waalikwa ninayo heshima kubwa sana ya kuwakaribisha

katika sherehe hii ya kumuaga binti yetu Upendo.” Alianza kuonyesha

mbwembwe zake huku akigeuka kumwangalia Upendo. Kisha akaendelea.

“Karibuni sana kuja kwenu ndo kumefanikisha sherehe hii. Kwa kuwa leo

ni siku ya furaha basi kila mtu afurahi kwa kadiri ya uwezo wake. Vyakula

ni vingi, vinywaji vimejaa, burudani kebekebe. Pia kutakuwa na

mashindano ya kucheza twisti kwa akina baba wenye vitambi (vicheko)

ambapo washindi watano wa kwanza watapewa zawadi na akina mama:

Mshindi wa kwanza atakabidhiwa kanga yenye ujumbe ulioandikwa

‘WALIONDANI WANATAMANI KUTOKA.’

Mshindi wa pili ‘atapewa kanga iliyoandikwa ‘WALIO NJE

WANATAMANI KUINGIA.’

Mshindi wa tatu atapata kanga yenye ujumbe ‘WADOGO

WANATAMANI UKUBWA.’

Mshindi wa nne atapewa kanga yenye maneno ‘WAKUBWA

WANATAMANI KURUDIA UTOTO.’ na

Mshindi wa tano ‘NDOA NDOANA’”





Aliongea MC huku akishangiliwa na umati wa watu na wengine

wakisimama na kwenda kwa Upendo kumrushia maua ya kila rangi. Ama

kweli MC alichangamsha sherehe vilivyo.

Upendo aliinama chini huku maua yakiendela kumwagwa alipokaa.

Alitafakari sana juu ya manjonjo ya MC kwani hakuelewa maana ya

ujumbe ulio katika zile zawadi watakazo kabidhiwa washindi wa twisti.

Sherehe iliendelea kupamba moto, muda ulifika wa kupata chakula huku

vinywaji vikisambazwa kila kona kwa fujo shughuli zote hizo

zikisindikizwa na muziki mwororo ulitumbuiza kwa sauti ya chini na ya

kubembeleza. Wakati kamati ya chakula ikijiandaa kuanza kugawa chakula,

ghafla MC alisimama mbele.

“Studio! Studio! Tafadhali!” MC alichombeza kumwashiria DJ azime

muziki ambaye naye alifanya hivyo mara moja. Kisha akaendelea.

“Wageni wetu waalikwa mabibi na mabwana. Mimi binafsi sitahesabia

kama shughuli hii imefanikiwa endapo Mchumba wa Upendo

hatutamtambua. Kwa hiyo nakuomba Upendo ututambulishe mchumba

wako kwa utaratibu nitakao kupangia.” Alishangiliwa MC hata kabla

hajamaliza kusema huku wengine wa kitamka neno kweli kwa sauti za juu.

James aliposikia hivyo, moyo ulimdunda alijua sasa muda wa kuumbuka

umefika. Alijikaza kiume na kusubiri kitakachotokea.

“Upendo njoo hapa!” Alitamka MC huku akiagiza aletewe glasi yenye

mvinyo na ua jekundu lililoandaliwa kwa shughuli hiyo. Watu wote

walitulia kimya mama mmoja mwenye mtoto aliyekuwa akilia alitoka naye

nje haraka sana ili kutoharibu utulivu. Upendo alipofika, MC akaendelea.

“Upendo!” Alitamka MC huku akimwonyesha ua na ile glasi yenye

mvinyo.

“Utakwenda wewe mwenyewe bila mpambe wako hadi alipo mchumba

wako. Ukifika mpe hili ua kama ishara ya upendo wenu wa kweli. Kisha

mpe huu mvinyo kama ishara ya kumkaribisha mchumba wako katika

maakuli kisha utamshika mkono na kumwongoza hadi katika meza ya

chakula, halafu utapakuwa chakula ambacho kitawatosha wote wawili

kisha utarudi kwangu ili niwaelekeze cha kufanya.” Alipomaliza tu

kuongea shangwe na vicheko viliibuka tena huku wengine wakimsifu MC

kwa umahiri alionao katika kumudu na kuipamba sherehe.

Upendo alikwenda kumtafuta mchumba wake huku ameshika vile vitu

alivyokabidhiwa na MC, alitembea kwa madaha yote asijue wapi amekaa

James aliangalia huku na kule lakini wapi hakumuona James. Baada ya

kuhangaika sana huku watu wakiwa na shauku ya kumwona James mwisho

akamwona amekaa katikati ya wazee aliokuja nao, aliongeza mwendo na

kwenda moja kwa moja hadi alipokuwa na kupiga magoti kisha akampa

lile ua huku akishangiliwa na kila mtu. Wengine wakitamka SAFI SANA!

UMECHAGUA!. Wakati Upendo akijiandaa kumpa James mvinyo kama

alivyoelekezwa na MC ghafla Eliza alipiga kelele ambazo zilimshtua kila

mtu.

“Nooooo! Hapana! Hapana! Juliasi!, Juliasi! Haiwezekani! Nasema

haiwezekani!” Yalimtoka maneno Eliza kwa mfululizo huku akirukaruka

kuelekea alipo James. Watu walijaribu kumshika lakini Eliza aliwazidi

nguvu, alikwenda hadi alipo James huku akitweta kama mtu aliyepandisha

mapepo.

“Kumbe wewe ni shemeji yangu?” Ilikuwa ni sauti ya Eliza mdogo wake

Upendo ambaye aliwafanya watu wamshangae ana matatizo gani. Ndipo

kabla hajaendelea kuzungumza alianguka na kuzimia.

Wazazi wake walishangaa nini kimetokea na huyo Juliasi ni nani.

“Kuna nini jamani mwanangu amekuwaje leo?” Aliuliza mama Upendo

huku akionyesha mshtuko mkubwa. Basi ndugu walimchukua na

kumpeleka ndani huku akipepewa.

Upendo alishindwa kuelewa kwa nini mdogo wake alitamka maneno yale,

basi alimshika James mkono.

“Mmh! Mdogo wangu atakuwa na matatizo makubwa sijui ana nini hebu

twende ndani tukamwone.” Alitamka Upendo huku wakiondoka kuelekea

ndani.

Wakati huo wote James alikuwa kimya kijasho chembamba kikimtoka kwa

kuogopa kilichotokea hivyo alishindwa kuongea chochote zaidi ya

kumfuata Upendo.

Walipoingia ndani walimkuta Eliza ameshazinduka. Alipomwona tu

James alisimama na kumshika kwa nguvu huku akilia kwa sauti ya juu.

“Kwa nini unafanya hivi? Unataka kutuangamiza mimi na dada yangu

Juliasi? Mimi nilikupenda sana na tayari nina mimba yako. Loh! Kumbe

ulikuwa una mwanamke tena dada yangu?” Aliongea Eliza kwa hasira na

hisia za ajabu huku Upendo akibaki anashangaa na kuuliza.

“Vipi Eliza mdogo wangu umechanganyikiwa? Huyu ni James sio Juliasi!”

Upendo alijaribu kumfariji mdogo wake.

“Sijachanganyikiwa dada yangu huyu bwana nilikutana naye Arusha

akaniambia kuwa anaitwa Juliasi. Naomba mmuulize mwenyewe aseme

ukweli.” Alisema Eliza kwa uchungu huku wazazi wake wakiwa hawaelewi

kinachoendelea.

Je, ni kweli anayosema Eliza?” Upendo aliuliza huku alimwangalia James.

James alikaa kimya kwa muda kisha alikaa chini kwenye kochi huku akiwa

ameinimisha kichwa chini kwa aibu na fedheha.

“Upendo yote aliyosema Esta ni kweli, naomba unisamehe ilikuwa ni

bahati mbaya sikujua kama ingekuwa hivi. Nisamehe mpenzi wangu

nilimfahamu Eliza kwa jina la Esta, siwezi kukupoteza nisamehe mpenzi.”

James aliomba na kukiri mbele ya wazazi wake Upendo na wazazi na

ndugu zake. James aliyasema hayo akiwa bado ameinama chini huku

machozi yakimlengalenga kwa aibu na hofu ya kumkosa Upendo.

“Hivi ninasikia au naota jamani, wewe James leo hii unanifanyia hivi? aibu

gani hii jamani? Angalia sasa umempa mimba mdogo wangu na mimi nina

mimba yako tayari hivi nifanyeje? James Mimi siwezi kukusamehe.”

Upendo aliongea kwa jazba huku amemkaba James shingoni kisha

akamwachia na kukimbilia nje.

Watu walimfuata ili kumshika lakini aliwazidi mbio na kutokomea gizani.

Sherehe ilivunjika, watu wote wakatawanyika kumtafuta Upendo. Upendo

alikimbia kwa mbio za ajabu kama mbwa mwenye kichaa, hakujali kabisa

kiumbe alichokuwa nacho tumboni. Wakati watu wanaanza kumtafuta

Upendo tayari alikuwa ameshafika mtaa wa tatu kutoka nyumbani kwao.

Baada ya kufika mtaa wa nne alikuwa tayari ameshafika katika barabara

kuu iendayo Msamvu, vile anaanza tu kukatisha barabara kulitokea baiskeli

iliyokuwa katika mwendo kasi ilimgonga na kumburuza hadi kwenye

mfereji. Upendo alilalamika sana kwa maumivu makali tumboni na

mgongoni. Wapitaji walisikia mtu akipiga kelele za nisaidieni kutoka katika

mfereji. Walifika na kumuinua na kumkalisha pembeni mwa barabara.

Wakati wakiendelea kumhoji kilichotokea wale watu waliokuwa wazazi

wake, James, Eliza na watu wengine walifika na kumkuta Upendo akiwa

hoi. Baba yake Upendo alimfukuza James na kutaka asionekane tena katika

familia ile ilikuwa ni aibu kubwa sana kwani furaha ilileta uchungu.

Upendo alikimbizwa katika Hospitali ya Mkoa wa Morogoro kwa

matatibu.

Huko hospitali hali ya Upendo ilizidi kuwa mbaya, mimba aliyokuwa nayo

iliharibika. Eliza alikuwa karibu naye wakati wote akimwomba msamaha

lakini Upendo alimfariji mdogo wake.

“Usijali mdogo wangu huna kosa mimi ndio mwenye kosa

sikukufahamisha shemeji yako. Lakini vilevile James hakuwa mwaminifu

alikuwa akinidanganya.” Upendo alisema maneno hayo kwa uchungu sana

huku machozi yakimtiririka mashavuni.

Baba na Mama yake Upendo walihuzunika sana wakiwaonea huruma

mabinti zao.

“Wanangu nawapenda sana haya mambo yameshatokea hakuna namna,

yule mwanamume ni muuaji sitaki kumsikia tena, kinachotakiwa ni

Upendo apone maisha yataendelea.” Baba Upendo aliongea huku

akimtazama mkewe.

“Ndio! Wanangu hii ni mitihani ya maisha, ni majaribu ila Mungu

atawasidia.” Mama Upendo aliongeza.

Kadiri siku zilivyokwenda Upendo aliendelea kuumwa sana. James maisha

yalianza kumwendea kombo, alikuwa amechanganyikiwa, siku zote alikuwa

ni mtu wa kujilaumu moyoni mwake akisema.

“Maisha yangu yamebadilika nimemkosa Upendo. Nimemkosea sana

Upendo na Mungu pia sistahili kusamehewa kabisa Mungu nisaidie.”

Aliongea James kwa kukata tamaa kabisa huku wazazi wake wakimwonea

huruma.

Siku moja wazazi wa James waliamua kumshauri James waende hospitali

kumwona Upendo ili akamwombe msamaha kwa mara nyingine.

Walipofika hospitali waliwakuta wazazi wa Upendo pamoja na watoto wao

wote wakiwa wamesimama wamekizunguka kitanda alipolala Upendo.

Walipoingia tu kabla hata hawajasalimia baba yake na Upendo alianza

kuwafukuza.

“Sitaki kuwaona hapa naomba mondoke yaani matatizo yote mnayotupa

hadi sasa bado mnakuja? James nasema ondokeni!” Alitamka baba

Upendo kwa hasira.

“Baba usiwafukuze wakaribishe nataka kuongea na James.” Alitamka

Upendo kwa taabu tena kwa sauti ya chini sana huku akinyoosha mkono

wa kulia akiashiria kumwita James.

“Utaongea naye nini yeye ndiyo chanjo cha wewe kuwa hapa leo nasema

watoke sitaki kuwaona hapa.” Alifoka baba Upendo.

Upendo aliendelea kusisitiza kuongea na James na aliwaomba wote watoke

nje abaki Eliza na James tu. Wote walitii na kutoka nje huku wakipigwa

na butwaa kwa nini Upendo amewafukuza.

James aliomba msamaha kwa Upendo akiwa amepiga magoti akijutia yote

aliyoyafanya. Pia James alimwomba msamaha Eliza kwa kumdanganya

kuwa hakuwa na mke wala mchumba. Eliza alimsamehe.

“James nitakusamehe lakini kwa masharti ya kwenda kuishi na mdogo

wangu Eliza mama mtarajiwa wa mtoto wako. Mimi sistahili tena kuwa

mke wako.” Aliongea Upendo huku akimkazia macho James na Eliza.

Kabla James wala Eliza hawajapata nafasi ya kujibu chochote, Upendo

aliyekuwa hoi kitandani aliinuka na kukaa kwa mara ya kwanza tangia afike

hospitali. James na Eliza walishangaa sana. Eliza pamoja na kushangaa

alifurahi kuona dada yake amekaa, alikwenda haraka nje kuwaita wazazi

wake na ndugu wa James ili waone maendeleo ya ghafla ya afya ya Upendo.

Huku akiwa amezungukwa na ndugu wa pande zote mbili Upendo

alitabasamu na kugeuka ili kumwangalia kila aliye kuwepo katika chumba

kile. Kisha Upendo alimshika mkono mdogo wake Eliza pamoja na

mkono wa James.

“Kama nilivyotoa masharti yangu nimekusamehe James, lakini kuanzia

sasa nenda mkaishi kwa furaha na amani na msahau yote yaliyotokea.

Uaminifu iwe nguzo ya upendo katika nyumba yenu. Mkaishi kwa

kumtegemea Mungu katika kila jambo.” Baada ya kuongea hivyo Upendo

akavuta mikono ya wote wawili kuelekea kifuani kwake kisha akaibusu na

kutamka maneno mawili tu “Nawapenda sana.”

Alipomaliza tu kuongea hivyo ghafla alipatwa na kwikwi na kukohoa kwa

nguvu huku akishindwa kupumua vizuri na kuangukia kitandani huku

akitupatupa miguu na mikono kama mtu mwenye kifafa na ghafla akatulia

na kufumba macho.

Eliza alikwenda haraka kumwita Daktari ambaye alifika na kumpima.

“Upendo amekata roho.” Yalikuwa ni maneno ya Daktari kutokana na

vipimo vyake.



MWISHO



HUU NI MWISHO WA KITABU CHA PILI KATIKA SIMULIZI YA MALIPO NI HAPAHAPA......

USIKOSE KITABU CHA TATU KINACHHOENDA KWA JINA LA “MAMA MDOGO”



TOA MAONI YAKO KUTOKANA NA KITABU HIKI CHA PILI......

0 comments:

Post a Comment

BLOG